Habari

Mpwa wa Bi. Kidude aishutumu Sauti za Busara kwa kumtelekeza shangazi yake

Mpwa wake na muimbaji mkongwe wa taarab wa visiwani Zanzibar, Bi. Kidude ameulaumu uongozi wa Busara Promotions kwa kile alichodai kumtelekeza shangazi yake.

Akiongea kwa uchungu kwenye kipindi cha Mimi na Tanzania cha Channel 10 kinachoendeshwa na Miss Tanzania, 1999, Hoyce Temu, alisema tangu Bi. Kidude aanze kusumbuliwa na maradhi mbalimbali yakiwemo ya kisukari, uongozi wa Busara umekuwa ukishindwa kutekeleza ipasavyo majukumu yake ya kumhudumia bibi huyo.

Alisema kwa kawaida Busara Promotions humlipa Bi. Kidude shilingi elfu 50 kwa wiki ili zimsaidie katika masuala mbalimbali lakini hela hiyo haijalipwa tangu mwezi August mwaka huu.

Aliongeza kuwa hivi karibuni Bi. Kidude alikuwa na hali mbaya hadi ikamlazimu amhamishie nyumbani kwake na gharama za matibabu yake huko Zanzibar yamekuwa yakitegemea fedha zake Bi. Kidude.

Alisema baada ya kuwa amezidiwa sana alijitokeza msamaria mwema wa jijini Dar es Salaam ambaye hakupenda kumtaja jina lake aliyewalipia nauli za ndege hadi Dar es Salaam na kulipia gharama za matibabu ya Bi. Kidude katika hospitali ya Hindu Mandal. Hiyo ilikuwa ni mwishoni mwa mwezi August mwaka huu ambapo watu walimzushia kifo.

Aliongeza kuwa baada ya kuruhusiwa na kurejea Zanzibar, msamaria mwema huyo aliwapigia simu na kuwaambia kuwa kuna watu walimpigia simu na kumtukana hivyo huo ndio ukawa mwisho wa kuwasaidia tena.

Tunajaribu kuutafuta uongozi wa Sauti za Busara kujibu suala hili.

Related Articles

Back to top button

Adblock Detected

Please don't block our ads, we rely on these ads to serve you with credible contents