Mr Touchez: Wasanii wanatunyonya sisi watayarishaji wa muziki
Mtayarishaji wa muziki kutoka Free Nation Sound, Mr Touchez amesema wasanii wanawanyima haki watayarishaji wa muziki katika nyimbo wanazoandaa.
Mr Touchez amewataka wadau mbalimbali wa muziki kutoa elimu juu ya haki miliki ili wajue thamani ya kazi wanayofanya.
“Unakuta msanii anafanya ngoma baada ya kumaliza anakimbia,” ameiambia Bongo5.
“Kwanza nawataka wadau mbalimbali kutoa elimu kwa wasanii. Wajue masuala haki miliki. Wasanii wanatakiwa kujua pesa wanayolipa studio ni pesa ya studio time, lakini ile kazi niliyofanya bado haijalipiwa, ni haki yetu sote. Mimi nashangaa, msanii anapeleka wimbo Mkito, kwenye mkataba kuna sehemu ya producer lakini unakuta wanasaini wenyewe, wanashindwa kujua hakuna msanii bila producer, wote tunategemeana na tuna haki ya kuendelea kunufaika na kazi tunazofanya,” amesisitiza.
“Mimi binafsi naitaka serikali kuangalia kwa makini suala la haki miliki. Ni hapa Tanzania tu, nchi kama Marekani producer kama Dr.Dre ni tajiri mkubwa duniani kuliko hata wasanii. Kwahiyo mimi naitaka serikali kuangalia hili suala kiumakini zaidi. Pia nawataka watayarishaji wenzangu tulizungumzie hili. Hata kama tusinufaike sisi kwa wakati huu lakini watayarishaji wa baadaye wanufaike na kazi zao.”