Mtoto wa kiume wa kinara wa madawa ya kulevya Mexico, El Chapo atekwa
Watu saba waliokuwa na silaha wamevamia kiota cha raha cha Puerto Vallarta kilichopo kwenye fukwe nchini Mexico na kumteka mtoto wa kiume wa mfanyabiashara maarufu wa madawa ya kulevya, El Chapo.
Kwa mujibu wa CNN, Jesus Alfredo Guzman, 29, mtoto wa – Joaquin “El Chapo” Guzman aliyepo jela, ametekwa pamoja na watu wengine sita Jumanne hii.
Utekwaji huo unakuwa pigo jipya kwa jitihada za Guzman akiwa jela kujaribu kuendeleza utemi wa cartel yake ya Sinaloa katika eneo hilo licha ya upinzani kutoka kwa kundi la Jalisco New Generation.
Jesus Alfredo na kaka yake Ivan Archivaldo Guzman wanasemekana kuendeleza shughuli za Sinaloa pamoja na mtoto wa El Capo aliyezaa na mwanamke mwingine, Ovidio Guzmán Lopez.
Jeshi la Mexico linaendesha msako wa kuwaokoa watu hao na kuwakamata wahusika. Jesus Alfredo ni mtoto mdogo kati ya watoto wawili wa El Chapo kwenye ndoa yake ya kwanza.
Kaka yake, Ivan Archivaldo Guzman, alifungwa Mexico mwaka 2005, lakini alitoka miaka miwili baadaye kutokana na kukosekana ushahidi.