Habari

Muigizaji Elizabeth Michael ‘Lulu’ atupwa jela miaka miwili

Muigizaji wa filamu nchini Tanzania, Elizabeth Michael maarufu kwa jina la Lulu amehukumiwa kifungo cha miaka miwili jela baada ya kukutwa na hatia ya kumuua aliyekuwa muigizaji mwenzake Steven Kanumba  bila kukusudia.

Lulu akiingia mahakani mapema leo jumatatu asubuhi

Akisoma hukumu hiyo leo Novemba 13, 2017, Jaji Sam Rumanyika amesema kuwa mshtakiwa alijikanganya kipindi akitoa ushahidi wake mahakamani kitu ambacho hata kama marehemu angefufuka leo mahakama hiyo isingeliweza kupokea ushahidi wa marehemu.

“Elizabeth Michael kwa mara kwanza alipelekwa Mahakama ya kisutu iliyopo Dar es salaam, akishtakiwa kuua bila kukusudia tarehe 7 mwaka 2012” – Jaji Rumanyika

“Katika ushahidi wa mazingira ambao mshtakiwa alikubali kwamba yeye ni mtu wa mwisho kuwa na marehemu ambapo mshtakiwa alikuwa na mahusiano na marehem kwa miezi 4” -Jaji Rumanyika

“Ushahidi wa mazingira unaweza kutumika kama msingi pekee wa kumtia hatiani mshtakiwa tena mshtakiwa pekee, Sasa ninapokwenda kuangalia maelezo ya mshtakiwa kama yanakidhi vigezo kama nilivyosema awali”-Jaji Rumanyika

“Kwa mujibu wa mshtakiwa alisema alianza kupigwa na marehemu, Mshtakiwa alisema kuwa marehemu alilewa lakini kuhusu mshtakiwa anatakiwa kutoa maelezo yanayo jitosheleza kwa hili mshtakiwa alijikanganya” – Jaji Rumanyika

“Mshtakiwa katika maelezo yake hakueleza kuwa marehemu alianguka au laah!! wakati anamkimbiza, Na maelezo ya Dkt. Josephine siyo maelezo ya cheti cha hospitali hayakuwa na hadhi ya hospitali”– Jaji Rumanyika

“Inakinzana na hekima ya kawaida kwamba hata pale marehemu alipoendelea kumpiga na kumshambulia na akaenda kiwango cha kumtishia kumuua, mshtakiwa hakuthubutu hata kumpiga ina maana alifanya kama maneno ya biblia yanavyosema MTU akikupiga shavu la kushoto mgeuzie la kulia lakini hili mshtakiwa hakulisema” – Jaji Rumanyika

“Hata kama marehemu angefufuka kwa miujiza Mahakama hii haitaweza kuchukua ushahidi wake.. Itoshe kusema kwamba mshtakiwa alisema marehemu alikuwa na wivu, wivu usiokuwa na mipaka” – Jaji Rumanyika

Baada ya kutoa maelezo hayo Jaji Rumanyika alisema kuwa Muigizaji wa filamu, Elizabeth Michael ‘Lulu’ amekutwa na hatia ya kuua bila kukusudia ambapo mawakili wa mshtakiwa walipewa muda wa kumtetea mshtakiwa mbele ya mahakama.

Wakili Msomi, Peter Kibatala ambaye ndiye wakili wa Lulu alisimama Mahakamani na kumtetea mteja wake kwa kusema kuwa Lulu haishi na wazazi wake wawili na ndiye msaada mkubwa kwa familia yake.

Baada ya utetezi huo ndipo mahakama ikatoa hukumu ya adhabu ya kifungo cha miaka miwili jela, ambapo kwa upande mwingine wakili wa Lulu, Peter Kibatala amesema watakata rufaa juu ya adhabu hiyo iliyotolewa na mahakama.

Related Articles

Back to top button

Adblock Detected

Please don't block our ads, we rely on these ads to serve you with credible contents