Mvua kubwa yaathiri usafiri Dar Es Salaam, Mamlaka ya Hali ya Hewa nchini (MET) yaendelea kutoa angalizo kwa wananchi
Mvua kubwa inayoendelea kunyesha katika mji wa Dar es Salaam, Tanzania imeathiri huduma ya usafiri wa umma huku idara ya hali ya hewa ikitoa tahadhari.
Kampuni ya Mabasi ya mwendo kasi (Udart) imelazimika kusitisha huduma zake usafiri kwa mabasi yanayotumia barabara kuu ya Morogoro eneo la Jangwani na barabara ya Kawawa katika Bonde la Mkwajuni kuelekea Morocco.
Taarifa ya Mkuu wa Idara ya Mawasiliano Udart, Deus Bugaywa imeeleza kuwa safari zilizositishwa ni kati ya Kimara -Kivukoni, Kimara – Gerezani, Morocco – Kivukoni na Morocco – Gerezani kuanzia mapema alfajiri ya leo Jumatatu.
“Huduma zinazotolewa sasa ni kati ya Kimara – Mbezi, Kimara -Magomeni Mapipa, Gerezani – Muhimbili, Kivukoni – Muhimbili na Gerezani – Kivukoni” amesema Buyagwa.
Eneo la Jangwani linafahamika kwa kujaa maji mengi barabarani kipindi cha mvua.
Udart wameomba radhi wateja wao na kuongeza kuwa wanaendelea kufuatilia hali ya maji Jangwani na kwamba yakipungua huduma zitaendelea kutolewa.
Baadhi ya watu wamekua wakitoa ushauri kwa wenzao walioshindwa kufika sehemu zao za kazi kutokana na changamoto ya usafiri ya kati kati ya mji kutumia usafiri mbadala.
Wengine waliamua kutumia mtandao wa kijamii wa Twitter kufanya hivyo.
How to get to Town (Posta) from Mbezi Mwisho.
Mbezi Mwisho – Ubungo = 2,000 Bajaji
Ubungo – Mwenge = 2,000 Bajaji
Mwenge – Makumbusho = 1000 Bajaji
Makumbusho – Posta = 3000 Bajaji
TOTAL = 8,000/=#MvuaZaMasika #MvuaZaDaresSalaam #MvuaDar pic.twitter.com/uI8na5Do84— Michael Marwa (@Kehongoh_Marwa) May 13, 2019
Ukiachana kutatizika kwa usafiri wa mwendokasi, wakaazi wengine wa maeneo mbalimbali ya Dar es Salaam wamekubwa na adha kubwa ya foleni kutokana na mvua hizo kuharibu ama kuziba baadhi ya barabara muhimu.
Mamlaka zaonya mvua kubwa
Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (MET) tayari imeshatoa tahadhari juu ya uwepo wa mvua kubwa ambayo itaupiga ukanda wa pwani wa nchi hiyo kwa siku tatu mfululizo kutokea leo Jumatatu Mei 13 mpaka Jumatano Mei 15.
Utabiri wa Hali ya Hewa wa saa 24 zijazo kuanzia saa 3 usiku wa leo 12/05/2019. Unaletwa kwenu na Godfrey Kazinja.#utabiriTZhttps://t.co/Ar6XaxcYiQ
— Tanzania Meteorological Authority (@tma_services) May 12, 2019
Utabiri wa Hali ya Hewa wa siku tano na athari zinazoweza kutokea. Umetolewa leo tarehe 12/05/2019 na Mamlaka ya Hali ya Hewa.#utabiriTZ pic.twitter.com/dASM78ChvX
— Tanzania Meteorological Authority (@tma_services) May 12, 2019
MET wametahadharisha kuwa mvua hizo zitakuwa na madhara makubwa ikiwemo: “Baadhi ya makazi kuzungukwa na maji, ucheleweshwaji wa usafiri, kusimama kwa muda kwa baadhi ya shughuli za kijami. Kuanguka kwa kwa majani na matawi ya miti. Kuathirika kwa usafiri wa baharini na uvuvi.”
Mamlaka hiyo pia imetahadharisha kuwa kwa siku za Alhamisi na Ijumaa wiki hii, ukanda huo wa pwani ya Tanzania utakabiliwa na upepo mkali.