Habari

Mwalimu anaswa akiishi na mwanafunzi kama mume na mke

Wananchi wa katika kijiji na kata ya Guta, wilaya ya Bunda mkoani Mara, wamelalamikia vitendo vinavyofanywa na baadhi ya walimu katika kata hiyo, kwa kufanya ngono na wanafunzi na kuishi nao kinyumba kama wake zao.

Hatua hiyo ya kulaani inatokana na hivi karibuni kumkamata mwalimu wa shule ye Msingi Guta, akiishi na mwanafunzi wa shule hiyo kinyumba kama mkewe.

Wananchi wa kata hiyo wakiongozwa na diwani wao, Kigo Nyamhanga, jana waliwaambia waandishi wa habari kwa njia za simu za mkononi kuwa hivi karibuni katika kijiji cha Guta, walifanikiwa kumkamata mwalimu huyo (jina linahifadhiwa) akiishi na mwanafunzi wa shule hiyo nyumbani kwake.

Wakizungumza kwa nyakati tofauti huku wakioneshwa kusikitishwa kwa vitendo hivyo, walisema kuwa baadhi ya walimu wa shule za msingi na sekondari, ambao hawazingatii maadili ya kazi yao, wamekuwa na tabia hiyo chafu na mbaya ya kufanya vitendo vya ngono na wanafunzi wao.

Walisema hivi karibuni saa za usiku walimkamata mwalimu huyo anayefundisha katika shule ya msingi Guta, akiwa na mwanafunzi mmoja wakiishi naye nyumbani kwake kama mke wake.

Walisema kuwa walifanikiwa kumtia mbaroni mwalimu huyo baada ya kupata taarifa kutoka kwa raia wema, kwamba mwalimu huyo anaishi na mwanafunzi huyo nyumbani kwake na wanafanya naye vitendo vya ngono. Walisema kuwa baada ya kumkamata polisi walifika na kumpeleka kituo kikuu cha polisi cha wilaya hiyo.

“Baada ya wananchi hao walioongoza na mwenyekiti wa kijiji chao walifanikiwa kumkamata live mwalimu huyo akiwa na mwanafunzi ndani ya nyumba yake” alisema mwananchi mmoja aliyejitambulsha kwa jina moja la Juma, mwenyekiti wa CCM, tawi la Guta.

Diwani wa kata hiyo, Kigo Nyamhanga, alithibitisha tukio hilo na kusema kuwa mwalimu huyo alikamatwa na wananchi walioongoza na mwenyekiti wa kijiji hicho.

Kufuatia tukio hilo, diwani huyo alikemea tabia hiyo na kuwataka walimu katika kata hiyo, kuachana na tabia hiyo chafu, kwani wao wanapewa watoto kuwalea na kuwafundisha na siyo kuwafanyia ukatili huo wa kijinsia huku akiongeza kuwa kamwe tabia hiyo katika kata yake, haiwezi kuvumiliwa ndani ya jamii na hata serikali kwa ujumla.

BY: EMMY MWAIPOPO

CHANZO: HABARILEO

Related Articles

Back to top button

Adblock Detected

Please don't block our ads, we rely on these ads to serve you with credible contents