Mwenyekiti wa Baraza la Katiba nchini Algeria, Tayeb Belaiz ajiuzulu
Mwenyekiti wa Baraza la Katiba nchini Algeria Tayeb Belaiz amejiuzulu wakati maelfu ya watu wamemininika mitaani kushinikiza kuondoka kwa washirika wote wa rais wa zamani Abdulaziz Bouteflika.
Shirika la habari la taifa APS limeripoti kuwa Belaiz amewasilisha barua yake ya kujiuzulu kwa rais wa mpito Abdelkadir Bensalah.
Maandamano yameendelea tangu kujiuzulu kwa Rais Bouteflika baada ya waandamanaji kuukataa uongozi wa Bensalah, Belaiz na waziri mkuu Noureddine Bedoui.
Mapema hapo jana maelfu ya wanafunzi waliandamana kwenye mitaa ya mji mkuu Algiers wakitaka kuondoka madarakani kwa viongozi hao.
Mnamo Aprili 9 Bensalah alichaguliwa na bunge kuongoza kipindi cha mpito cha miezi mitatu kufuatia kujiuzulu kwa Rais Bouteflika kulikosababishwa na maandamano dhidi ya utawala wake wa miaka 20.