Wanadiplomasia wa India na China wamekutana mjini Beijing kuzungumzia mzozo unaozidi makali, baada ya uamuzi wa serikali ya mjini New Delhi wa kubatilisha kanuni za jimbo la Kashmir, ambalo China pia inadai kumiliki sehemu ya jimbo hilo.
Shirika rasmi la habari la China Xinhua limesema waziri wa mambo ya nchi za nje Wang Yi amemwambia waziri mwenzake wa India Subrahmanyam Jaishankar jana mjini Beijing kwamba China inataraji India itatoa mchango wa maana katika kudhamini utulivu na amani katika eneo hilo.
Shirika la habari la Xinhua limemnukuu waziri Jaishankar akisema “India itaendelea kuheshimu makubaliano yaliyofikiwa pamoja na China ya kusaka ufumbuzi wa suala la mpaka kwa njia ya mazungumzo. India na China zilipigana vita mwaka 1962 kuhusu eneo la mpakani la Kashmir.
Chanzo shirika la habari la DW.