Ndege yatua ghafla baada ya kuhisiwa kuwa na vilipuzi
Ndege moja iliokuwa ikitoka Krakow kuelekea mjini Dublin ililazimika kutua ghafla baada ya kutoa alam ya iliyoashiria kuwepo na vilipuzi ndani ya choo.
Ndege hiyo ya kampuni ya Ryanair ilibadili mwelekeo hadi katika uwanja wa ndege wa Stansted ambapo maafisa wa polisi wa Essex wanaikagua.
Hata hivyo ndege mbili za kijeshi ziliisindikiza ndege hiyo ambayo ilitua mwendo wa saa kumi na mbili.
Msemaji wa ndege hiyo alisema ndege hiyo ilitua vizuri lakini ilipelekwa hadi katika eneo la mbali ambapo abiria walishuka salama.
Kanda ya video ya RAF ilikuwa ikisambazwa. Andy Kirby kutoka Essex alisema ”Inaonekana kama ndege za kijeshi za eurofighters zilikuwa zikizunguka juu ya nga ya uwanja wa ndege wa Stansted.”
Msemaji huyo wa Ryanair aliongezea katika taarifa kwamba ”Ndege hiyo na abiria wake wanachunguzwa na maafisa wa polisi wa Uingereza ambao wataamua iwapo wataendelea na safari yao ya kuelekea mjini Dublin kwa kuwekwa kwenye ndege nyengine.
”Abiria mjini Dublin wanao subiri kuelekea Krakow wanaingizwa katika ndege tofauti ili kupunguza uwezekano wa kuchelewa.”
Maafisa wa polisi wa Essex walisema ”Tumefanikiwa kuwatoa abiria wote kutoka katika ndege hiyo. Ndege hiyo hadi kufikia sasa imetengwa katika uwanja wa ndege wa Stansted na uchunguzi wetu unaendelea”.