Michezo

Niliitwa ‘Simba wa Yuda’ kwa sababu Yanga walikwenda kunishitaki CAF – Mwina Kaduguda

Aliyekuwa kiongozi wa soka Tanzania na Katibu Mkuu wa Simba, Mwina Kaduguda ameelezea chanzo cha kupewa jina lake la utani la ‘Simba wa Yuda’.

Kaduguda amezungumzia chanzo cha jina hilo la Simba wa Yuda wakati alipofanya mahojiano na Azam tv kupitia kipindi cha Nyundo ya Baruan Muhuza.

”Hili jina mimi nimepewa na kusema ukweli nilijaribu kulikataa lakini jamii ikishaamua jambo lake basi huna jinsi ya kulizuia. Mimi niliingia TFF wakati huo FAT kulikuwa na matatizo, viongozi wawili wa juu walikuwa wanagombana wakafikia mahala pakuweka hadharani, Mwenyekiti akasema mimi siwezi kufanya kazi na katibu na katibu vile vile akaja mbele ya vyombo vya habari na kusema mimi siwezi kufanya kazi na Mwenyekiti,” amesema Kaduguda.

Kaduguda ameongeza ”Sasa watu wenye chama chao wakati ule walisema basi waturudishie chama chetu kama hawa wamekiri hadharani hawa wezi kufanya kazi pamoja. Wenye chama wakati ule ilikuwa ni viongozi wote wanaoongoza mpira katika Mikoa ya Tanzania bara ambao ni mkutano mkuu wa nchi nzima ukakutana Dodoma kwa hiyo wakachagua uongozi wa mpito ili utengeneze uchaguzi na ndipo nilipo ingia.”

”Wakati mimi naongoza TFF ikiwa (FAT), nilikuta imebaki michezo mitano kwenye ligi kabla ya kulizika na wakati ule Simba ilikuwa bingwa wa nchi na wakati ule klabu ngumu kama Azam na Mtibwa leo ni Tanzania Prisons, Ruvu JKT.”

”Kwa hiyo Yanga ilikuwa inacheza mechi yao Tanga mimi nikiwa mgeni kabisa watu wanaskia Kaduguda lakini hawanijui na siku hiyo nilikuwa kwenye mechi nime kaa jukwaa la Urusi Mkwakwani sasa watu wanaongea Kaduguda naskia ni mtu mkali mimi nawaskia nimekaa nao lakini hawanijui.”

”Kwa hiyo Yanga walitakiwa washinde goli moja tu wawe mabingwa wa nchi lakini mpaka mapumziko Yanga imepigwa goli 2 – 0 na baadae wakatoka 2 – 2. Na walikuja kuniomba mimi niwasaidie Yanga wawe mabingwa ni kasema mimi siwezi kuwasaidia kwa kwenda kucheza ila nitawasaidi kwa kuweka mazingira ya kiufundi.”

”Wakashindwa kuwa mabingwa kwa matokeo hayo Yanga wakanishitaki mahakamani kwamba nimewahujumu mimi ni Simba kumbe matatizo ni yao.”

”Jina la ‘Simba wa Yuda’ niliitwa kwa sababu Yanga walikwenda kunishitaki CAF kwa hiyo ikasemekana Tanzania imeondolewa kwenye mashindano waandishi ikawa kila siku wanajaa kwenye ofisi za chama cha soka Tanzania (FAT).”

”Watu walikuwa wakinishutumu na kuniona kama vile nimeiingiza nchi kwenye matatizo na mwisho wasiku niliteuwa Simba na Mtibwa waende kushiriki michuano ya kimataifa. Kwa hiyo niliitwa kwa sababu mwisho wa siku Simba ilicheza ubingwa wa Afrika na Mtibwa ikafanikiwa kucheza kombe la CAF.”

Mwina Kaduguda ‘Simba wa Yuda’ ambaye ni msomi wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam kwa sasa ni mwalimu katika shule ya Sekondari, Jitegemee jijini Dar es Salaam.

Related Articles

Back to top button

Adblock Detected

Please don't block our ads, we rely on these ads to serve you with credible contents