Nyota ya Ole Solskjaer yaendelea kung’ara EPL, ni mwendo wa dozi tu
Nyota ya kocha wa muda wa Manchester United, Ole Gunnar Solskjaer imeendelea kuwaka akiwapa ushindi mfululizo wekundu hao wa Old Trafford unaokausha vidonda vya vipigo walivyokuwa wakivipokea.
Jana, Manchester United ikiongozwa na Solskjaer ilifanikiwa kugawa kipigo cha 2-0 dhidi ya Newcastle United na kuandika historia ya aina yake.
Kutokana na ushindi huo wa jana, Solskjaer amekuwa kocha wa kwanza wa klabu hiyo tangu miaka 72 iliyopita, kufanikiwa kushinda michezo yake ya kwanza minne mfululizo kwenye mechi za Ligi Kuu ya Uingereza.
Kocha huyo ambaye ana historia ya kufanya maajabu akiichezea klabu hiyo miaka kadhaa iliyopita, ameifuata rekodi ya kocha pekee wa Manchester, Sir Matt Busby ambaye aliweka rekodi hiyo mwaka 1946.
Magoli ya Manchester United jana yalifungwa na Romelu Lukaku katika dakika ya 64 akitokea benchi pamoja na Rashford aliyefunga jalada la hukumu ya siku katika dakika ya 80.