Habari

Papa Francis awatambua na kuwaridhia maaskofu saba walioteuliwa China

Papa Francis awatambua na kuwaridhia maaskofu saba walioteuliwa China

Makao makuu ya Kanisa Katoliki, Vatican na China zimetangaza juu ya kutiwa saini mkataba wa kihistoria, wa muda mfupi uliofikiwa kati ya pande hizo mbili kuhusu uteuzi wa maaskofu nchini China.

Papa Francis amekubali uhalali wa maaskofu saba wa China, walioteuliwa na China bila idhini ya Vatican. Hatua hiyo imemaliza mzozo wa kidiplomasia uliokuwepo kwa miongo kadhaa na ambao umesababisha mgawanyiko miongoni mwa waumini wa Kikatoliki nchini China. Ni miongo saba sasa tokea Vatican na China zikate mahuasiano rasmi kati yao.

Uamuzi huo ni sehemu ya makubaliano ya kihistoria kati ya Kanisa Katoliki na China juu ya uteuzi wa maaskofu, jukumu ambalo kwa kawaida huwa la Papa. Mkataba huo wa muda ulisainiwa mjini Beijing na kutangazwa wakati Papa Francis alipokuwa anafanya ziara nchini Lithuania ikiwa ni mwanzoni mwa safari yake ya siku nne katika mataifa yanayoizunguka bahari ya Baltic, kaskazini mwa Bara la Ulaya.

Kwa mujibu wa taarifa kutoka Vatican, Papa Francis anatarajia, kwamba maamuzi haya, yataweka chachu katika mchakato mpya utakaoanzisha ushirikiano kamili wa Wakatoliki wote wa nchini China na ambao utafunika majeraha ya zamani.

Kwa muda wa miezi kadhaa ripoti za vyombo vya habari zimekuwa zikisema kwamba Papa Francis alikuwa tayari kukubali uhalali wa maaskofu waliochaguliwa na serikali ya China ili kurejesha uhusiano wa kidiplomasia kati ya Beijing na Vatican, uliokufa tangu  mwaka 1951.

Jarida la nchini Marekani la Wall Street liliripoti mapema mwaka huu kuwa mamlaka ya China ingeweza kumpa uwezo papa kuhusu jukumu la kuteua maaskofu hapo baadaye, ingawa hili halijahakikishwa bado.

Chini ya mkataba huo, maaskofu mawili wanaotambuliwa na papa, wameombwa na mwanadiplomasia wa juu wa Vatican wajiuzulu ili kuwapa nafasi maaskofu waloteuliwa na serikali.

Wakatoliki milioni 12 nchini China wanaunda idadi ndogo ya jumla ya watu bilioni 1.4 nchini humo. Mamilioni wameendelea kuwa waaminifu kwa makao makuu ya kanisa katoliki, Vatican licha ya serikali ya China kuanzisha Kanisa Katoliki linalosimamiwa na serikali tangu mwaka 195, ambapo serikali imekuwa inateua maaskofu wake tangu wakati huo.

Wengi wa waumini wa kanisa Katoliki linaloongozwa na Vatican wamelazimika kuendesha ibada zao chini kwa chini, na wamekuwa wakikabiliwa na unyanyasaji na kifungo. Makundi ya kutetea haki za binadamu yameuita mkataba huo kuwa ni sawa na Vatican imenunuliwa kwa bei nafuu na China wakati ambapo nchi hiyo inakabiliwa na lawama za ukandamizaji mkubwa wa Ukristo kwa miaka mingi.

Rais wa China Xi Jinping anajaribu kuzifanya dini zote nchini China ziwe na sifa moja ya kuithamini nchi hiyo kama vile kuwa na utiifu kwa chama cha Kikomunisti. Miezi michache iliyopita, mamlaka za serikali za mitaa nchini China ziliyafunga mamia ya makanisa na nyumba binafsi zilizotumiwa kama makanisa.

Chanzo DW

By Ally Juma.

Related Articles

Back to top button

Adblock Detected

Please don't block our ads, we rely on these ads to serve you with credible contents