Picha: ACT – Wazalendo watua Kata ya Kijichi kumnadi mgombea wao
Chama cha ACT – Wazalendo kimeendelea na kampeni zake kwenye Kata ya Kijichi kwa kumnadi mgombea Wa Kata hiyo,Edger Mkosamali nyumba kwa nyumba.
Akizungumzia wakati wa Kampeni hizo katika Kata hiyo, Katibu Wa Itikadi, Mawasiliano na Uenezi Wa ACT- Wazalendo Ndugu Ado Shaibu amesema kuwafikia watu majumbani kunawapa fursa ya kufafanua vyema ujumbe wetu wa kampeni.
Kampeni za udiwani zilishafunguliwa, kwenye kata 43 ambazo zitarudia uchaguzi kutokana na Viti vya madiwani kuwa wazi kutokana na sababu mbalimbali ikiwemo vifo, kujiuzulu na kutenguliwa na mahakama.
“Kuwafikia watu Majumbani kunatupa fursa ya kufafanua vyema ujumbe wetu wa kampeni. Ujumbe wetu ni UCHUMI na HAKI. Wananchi wanatupokea vizuri. Ingawa serikali inahaha kutuzuia tunapoweka bayana jinsi uchumi ulivyosinyaa, mitaani kumejaa mifano chungu tele ya kudorora kwa uchumi. Njia hii ya nyumba kwa nyumba inawapa pia fursa wananchi ya kuhoji mambo mbalimbali kuhusu chama na mgombea wetu na kupata majibu hapo hapo” amesema Ado.