Polisi aliyeua Magereza atinga kortini
Askari polisi anayedaiwa kumuua askari Magereza kwa kummiminia risasi 21 mkoani Manyara na kufukuzwa kazi, amefikishwa mahakamani akikabiliwa na shtaka la mauaji.
Na Charles Masayanyika, PST Babati
Askari polisi anayedaiwa kumuua askari Magereza kwa kummiminia risasi 21 mkoani Manyara na kufukuzwa kazi, amefikishwa mahakamani akikabiliwa na shtaka la mauaji.
Askari huyo, E. 2821, Konstebo Martin Lufungilo (38), mkazi wa mtaa wa Majengo mjini hapa, anadaiwa kumuua kwa kumpiga risasi kichwani, askari wa Gereza la Wilaya ya Babati.
Mtuhumiwa huyo alifikishwa juzi katika Mahakama ya Hakimu Mkazi mkoani Manyara akiwa katika gari aina ya Land Rover 110 Defender T990AAB iliyokuwa doria siku ya mauaji hayo huku ikiwa imetobolewa na matundu ya risasi kwenye vioo na ubavuni.
Alisindikizwa na Ofisa Upelelezi wa Mkoa Manyara, Bw. Japhet Mwingira.
Baada ya kufikishwa mahakamani, alipandishwa kizimbani na kusomewa shtaka la mauaji.
Shtaka hilo lilisomwa na Inspekta Ralph Meela, mbele ya Hakimu Mkazi Mfawidhi Mwandamizi, Huruma Shaidi.
Inspekta Meela alidai kuwa, mshitakiwa alitenda kosa hilo Februari 24, mwaka huu, saa 1:14 usiku katika eneo la Kata ya Maisaka `A`, kwa kumpiga risasi na kumuua askari wa Magereza A. 1557 Sajenti James Ngolo.
Mshtakiwa alipelekwa katika gereza la Babati hadi kesi hiyo itakapotajwa tena Machi 13, mwaka huu.
Source: Nipashe