Rais Donald Trump achukizwa na kauli ya kuitwa ‘MZEE’ na Korea Kaskazini
Wakati vita vya maneno vikiendelea kati ya Rais wa Marekani, Donald Trump na Kiongozi wa Korea Kaskazini, Kim Jong-un inaonekana Trump kuguswa zaidi na kauli zilizotolewa jana na serikali ya Korea Kaskazini kwa kumuita kuwa ‘mzee na mchochezi wa vita’ kitu ambacho kimemfanya aweke wazi hisia zake kuwa angefurahi siku moja kuona wanakaa meza moja na Kim .
Wizara ya mashauriano ya nchi za kigeni nchini Korea Kaskazini jana ilimuita Trump kuwa “mchochezi wa vita na mzee” na kusisitiza kuwa haiwezi kamwe kuachana na mipango yake ya kutengeneza silaha za nyuklia.
Kauli ambayo Rais Donald Trump alishindwa kujizuia kuijibu kwa kuandika kwenye ukurasa wake wa Twitter kuwa, anashangaa ni kwa namna gani Kiongozi wa Korea Kaskazini anamuita mzee wakati yeye hata siku moja haijawahi kutokea kumkebehi kuwa mfupi na mnene.
“Kwanini Rais Kim Jong-un ananitukana kuwa mimi ni mzee wakati mimi hata siku moja sijawahi kumuita yeye mfupi na mnene? Sawa najaribu kila niwezalo kuwa rafiki yake najua ipo siku tutakuwa marafiki.“ameandika Rais Donald Trump.
Why would Kim Jong-un insult me by calling me "old," when I would NEVER call him "short and fat?" Oh well, I try so hard to be his friend – and maybe someday that will happen!
— Donald J. Trump (@realDonaldTrump) November 12, 2017
Hata hivyo huenda Rais Trump amesahau kwani awali alinukuliwa akimkejeli kiongozi huyo mkuu wa Korea Kaskazini, kwa kumuita mwendawazimu na ‘mtu wa kuunda zana za roketi’.
Hatua hiyo ya Rais Trump kujibu kauli ya Korea Kaskazini imezua gumzo nchini Marekani wengi wakimuona Trump kama Rais anayeongoza taifa hilo kubwa duniani kwa mzaha.