Habari

Rais Magufuli afunguka kuhusu Corona “Tunatishana mno”

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli amewataka Watanzania kutotishwa na janga la ugonjwa wa homa ya mapafu inayosababishwa na virusi vya Corona (Covid-19) na badala yake waendelee kuchapa kazi na kujenga uchumi huku wakizingatia tahadhari zote za kujikinga kuambukizwa ugonjwa huo kama zilivyotolewa na wataalamu.


Mhe. Rais Magufuli amesema hayo tarehe 22 Machi, 2020 alipohudhuria Ibada ya Jumapili katika Kanisa la Mtakatifu Paulo wa Msalaba, Jimbo Kuu la Jimbo Kuu Katoliki la Dodoma, iliyoongozwa na Paroko wa Parokia hiyo Padre Onesmo Wisi.

Katika salamu zake katika Ibada hiyo, Mhe. Rais Magufuli amesema kuwepo kwa ugonjwa wa Corona isiwe sababu ya kutishana kiasi cha kumsahau Mwenyezi Mungu, hivyo ametoa wito kwa Wakristo na Waumini wa madhehebu mengine kumrudia Mwenyezi Mungu ili aepusha janga hili, badala ya kumwacha shetani atawale.

Mhe. Rais Magufuli amekemea tabia za baadhi ya watu wanaofanya mzaha juu ya ugonjwa huu ama kuwatia hofu wananchi kupitia vyombo vya habari na mitandao ya kijamii, na badala yake ametaka Watanzania waendelee kuchapa kazi huku wakizingatia tahadhari.

“Watu tusitishane, tunatishana mno. Niwaombe ndugu Wakristo na Watanzania kwa ujumla wa Madhehebu yote, huu ndio wakati mzuri sana wa kumtegemea Mungu kuliko wakati wote, tuendelee kuchapa kazi, tuendelee kuujenga uchumi wetu, hatuwezi kusalimu amri kwa ugonjwa huu wa Corona na kushindwa kumtegemea Mungu na tukashindwa kuendeleza uchumi wetu” amesema Mhe. Rais Magufuli.

Amewashukuru viongozi wa Dini kwa kuungana na Serikali katika kuwahamasisha wananchi kuchukua tahadhari na ametoa wito kwa viongozi hao kuendelea kuliombea Taifa ili Mwenyezi Mungu aepushe balaa hili la Corona.

Related Articles

Check Also
Close
Back to top button

Adblock Detected

Please don't block our ads, we rely on these ads to serve you with credible contents