Habari

Rais Magufuli asamehe wafungwa 4,477 kuelekea sherehe ya Uhuru

Rais John Magufuli amerejea kauli yake ya kuahirisha  maadhimisho ya sherehe za uhuru zinazofanyika Desemba 9 kila mwaka na kuagiza fedha zilizotengwa zielekezwe kujenga hospitali jijini Dodoma itakayoitwa Hospitali ya Uhuru.

Akizungumza leo Ijumaa Desemba 6, 2018 wakati akitoa salamu za siku ya Uhuru Ikulu, Dar es Salaam, Rais Magufuli pia ametoa msamaha kwa wafungwa 4,477 ambapo kati yao 1,176 wataachiwa huru siku ya maadhimisho hayo.

Novemba 20, 2018 Waziri Mkuu Kassim Majaliwa alieleza kuwa Rais Magufuli ameagiza Sh995.182 milioni zilizokuwa zimetengwa kwa ajili ya kufanikisha sherehe hizo zitumike kwa ajili ya ujenzi wa hospitali hiyo.

Majaliwa alitoa kauli hiyo alipokutana na viongozi waandamizi wa mkoa wa Lindi.

“Ili kutekeleza mawazo ya waasisi wetu Serikali imeamua kuhamishia rasmi makao makuu ya nchi yetu jijini Dodoma na karibu wahusika wengi wameshahamia kule, nimebaki mimi ambaye nina mpango wa kuhamia hivi karibuni,” amesema Magufuli leo.

“Hii imefanya mahitaji ya huduma ya jamii ikiwamo afya katika jiji la Dodoma kuongezeka. Hivyo tumeamua kujenga Hospitali nyingine kubwa itakayosaidiana na hospitali ya Benjamini Mkapa na Hospitali ya Mkoa wa  Dodoma.”

Amesema hospitali hiyo itakayoitwa itasaidia kuongeza kasi ya utoaji wa huduma za afya jijini hapo.

Kuhusu msamaha wa wafungwa amesema utawahusu wafungwa wagonjwa, wazee, wafungwa wa kike walioingia gerezani wakiwa wajawazito, walioingia watoto wanaonyonya na wasionyonya  pamoja na wafungwa wenye ulemavu wa mwili na akili.

“Hali kadhalika nimeamua kwa wafungwa waliotumikia robo ya adhabu zao wapunguziwe robo ya adhabu zao baada ya punguzo la kawaida la theluthi moja linalotolewa kwenye kifungu cha 49 (1) cha Sheria ya magereza Sura ya 58,’ amesema rais Magufuli.

Related Articles

Back to top button

Adblock Detected

Please don't block our ads, we rely on these ads to serve you with credible contents