Habari

Rais Magufuli atoa wito kwa Taasisi za kibenki nchini

Rais wa Jamhuri Ya Muungano wa Tanzania, Dkt.John Pombe Magufuli ametoa wito kwa Taasisi za kifedha nchini kupunguza riba kwenye mikopo ili wananchi wa kawaida waweze kukopa na kukuza mitaji yao.

Wito huo ameutoa leo, wakati akizungumza na wananchi wa Wilaya ya Chato, Mkoani Geita katika shughuli za ufunguzi wa tawi la benki ya CRDB lililopo mjini Chato.

Rais Magufuli amesema kuwa, Ni muhimu Taasisi za kifedha kupunguza riba ili kuwafaa wananchi, kwa sababu wengi wao huogopa kukopa na hivyo kuathiri maendeleo ya watu hao na taifa, hususani kwenye kipindi hiki cha kuijenga Tanzania kuwa ya viwanda.

“Naiomba Benki kuu ya Tanzania na benki zingine kupunguza riba kwa wananchi,ili wananchi wa kawaida hata masikini waweze kukopa na kuweka mitaji yao midogo kwa ajili ya maendeleo yao na ya taifa kwa ujumla”, alisema Rais Magufuli.

Aidha ,Rais Magufuli ametahadharisha kuwa, hakuna sababu ya kuwa na benki nyingi ambazo hazihudumii wananchi kwa ufanisi na badala yake amesema ni bora ziwepo chache ambazo zitafanya kazi za kuwanufaisha wananchi bila upendeleo ili waweze kusimama na kujiendeleza.

“Benki ni kama biashara nyingine, ukiwa na duka ukaliendesha vibaya likafilisika, utalifunga, utabaki na nguzo tu,kwa hiyo na benki ni chombo chochote kinachofanya biashara, ukikiendesha vibaya lazima kife”, alisisitiza Rais Magufuli.

Hata hivyo,Rais Magufuli amewataka kwa wananchi kuwa wazalendo kwa kuweka fedha zao kwenye benki zilizopo nchini, ili kuongeazea mitaji na kuzikuza kiuchumi badala ya kuwekeza nje.

Related Articles

Back to top button

Adblock Detected

Please don't block our ads, we rely on these ads to serve you with credible contents