Rais wa Marekani Donald Trump amepokelewa na maandamano huko Dayton Ohio siku nne baada ya shambulizi lililofanywa na mtu aliyejihami kwa bunduki kuwauwa watu.
Trump pamoja na mke wake Melania wametembea hospitali moja mjini humo ambapo baadhi ya wahanga wa shambulizi hilo wanapokea matibabu.
Kwa mujibu wa shirika la habari la DW, Karibu na hospitali hiyo mamia ya watu walikuwa wanaandamana barabani wakipinga ziara hiyo ya Trump. Waandamanaji hao walikuwa wamebeba mabango yaliyomtaka rais huyo kukishinikiza Chama kinachotetea umiliki wa bunduki Marekani NRA kusitisha uuzaji wa silaha hizo.
Kabla hapo Trump alikuwa ametembelea eneo la El Paso huko Texas ambapo watu 22 waliuwawa na mtu mwengine aliyekuwa amejihami kwa bunduki. Ubaguzi wa rangi unadaiwa kuwa kichochea cha shambulizi hilo.