Habari

Raisi wa Urusi Vladimir Putin aupiga vita muziki wa kurap ‘Kufoka foka’ aitaka serikali iudhibiti

Rais wa Urusi Vladimir Putin ameitaka serikali yake “kuchukua uongozi” wa muziki wa kufoka foka ama rap. Japo matamasha kadhaa ya muziki huo yamezuiwa katika maeneo mbalimbali ya nchi hiyo katika siku za hivi karibuni, jitihada za serikali kuupiga marufuku kabisa zimegonga mwamba. Sababu marufuku ya serikali imeshindikana, Putin anataka mamlaka zifanye kazi ya ziada kuudhibiti. “Wizara ya Utamaduni itatafuta namna bora ya kusimamia matamasha ya vijana,” amesema Putin.

Kauli ya Putin inakuja siku chache baada mwanamuziki wa maarufu wa rap nchini humo anayefahamika kama Husky kukamatwa baada ya matamasha yake kufutwa. Awali mwezi huu wa Disemba mamlaka katika jiji la kusini la Krasnodar zilizuia tamasha la Husky kwa kile walichokiita “msimamo mkali”.

Mwanamuziki huyo ambaye jina lake halisi ni Dmitry Kuznetsov – alikonga nyoyo za mashabiki wake kwa kutumbuiza kutoka juu ya gari. Hata hivyo alikamatwa na kufungwa jela kwa siku 12 kwa kitendo hicho.

Mwanamuziki wa Rap nchini Urusi Dmitry Kuznetsov maarufu kama Husky amekuwa akikabiliana na mamlaka kila uchao

Akizungumza katika mkutano wa Baraza la Utamaduni na Sanaa katika jiji la St Petersburg, rais Putin amesema “tatizo hili linapaswa kutatuliwa kwa umakini mkubwa”. “Kile ambacho ninakubaliana nacho ni kuwa, kama ni ngumu kuuzuia (muziki wa rap), basi inabidi uongozwe kwa namna yake,” amesema.

Putin ameelezea khofu yake juu ya matumizi ya mihadarati kwa vijana. “Rap na aina nyengine za kisasa za sanaa zimejikita katika nguzo tatu- ngono, mihadarati na maandamano,” amesema Putin na kuongeza:”Ninaogopa zaidi mihadarati, maana hiyo ndio njia ya kuangamiza taifa.”

Putin amelalamikia lugha chafu inayotumika kwenye rap, na kusema amezungumza suala hilo na mtaalamu wa lugha.

Japo mtaalamu huyo alimwambia kuwa matusi ni “sehemu ya lugha yetu”, Putin alifananisha suala hilo na mwili wa binadamu, huku akitania kuwa “tuna viungo vya kila aina, lakini hatuvuachi wazi kila wakati”. Serikali ya Urusi imekuwa na mahusiano ya kutatanisha na muziki kwa muda mrefu.

Bendi ya muziki ya Pussy Riot ambayo ni maarufu kwa kuukosoa utawala wa Putin imedai kuwa shirika la ujasusi la nchi hiyo lilimdunga sumu mwana bendi hiyo Pyotr Verzilov mwezi Septemba mwaka huu.

Pyotr Verzilov akipelekwa mahakamani baada ya yeye na wanabendi wenzie wa Pussy Riot kuvamia uwanja kwenye fainali ya Kombe la Dunia nchini Urusi mwezi Julai 2018.

Chini ya Usovieti, aina za muziki za Magharibi kama pop na rock zilikuwa ni marufuku na baadhi ya wanamuziki wa Kirusi waliofanya aina hizo za muziki walikabiliana na mkono wa sheria. Hata wale waliofanya muziki wa asili pia waliingia kwenye migogoro na serki. Mwanamuziki Dmitri Shostakovich alipigwa marufuku mara mbili chini ya utawala wa Joseph Stalin.

By Ally Juma.

 

Related Articles

Back to top button

Adblock Detected

Please don't block our ads, we rely on these ads to serve you with credible contents