RIPOTI: Hii ndiyo idadi kamili ya watu Tanzania, Yakimbizana na Afrika Kusini
Ripoti ya makadirio ya watu nchini iliyozinduliwa leo Jumatano Februari 28, 2018 na Waziri wa Fedha na Mipango, Dkt. Phillip Mpango inaonyesha Tanzania kuna idadi ya watu milioni 54.2 hadi kufikia mwaka 2018, ambapo imeelezwa kila mwaka kuna ongezeko la watu milioni 1.6.
Ripoti hiyo inaonyesha Tanzania Bara kuna watu milioni 52.6 na Visiwani Zanzibarkuna watu milioni 1.6 . kwa matokeo ya ripoti hiyo inaifanya Tanzania kuwa nchi ya sita barani Afrika kwa ongezeko kubwa la watu ikitanguliwa na Nigeria, Ethiopia, DR Congo, Misri na Afrika Kusini.
“Ongezeko hili linatokana na idadi kubwa ya vizazi vipatavyo milioni 2 ikilinganishwa na idadi ndogo ya vifo ambavyo nintakribani 400,000 kwa mwaka,” amesema Waziri Mpango.
Kwa upande mwingine, Waziri Mpango ameyaonya mashirika na watu binafsi kutokutoa takwimu zozote bila kushirikisha Ofisi ya Taifa ya Takimu (NBS) kwani kufanya hivyo ni kosa kisheria.
Aidha, Ripoti hiyo imeonesha makadirio kuwa Tanzania itakuwa na watu milioni 77.5 ifikapo mwaka 2018 wakati ambapo nchi zote duniani zitakuwa zinatathmini mafanikio na changamoto za Malengo ya Mpango wa Dunia wa Maendeleo Endelevu (SDGs).
Ofisi ya Taifa ya Takwimu (NBS), awali kupitia kwa Mkurugenzi wake Dkt. Albina Chuwa amesema kuwa kasi hiyo kubwa ya ongezeko la watu inasababishwa na kiwango cha juu cha uzazi ambapo tafiti zinaonyesha wastani wa mwanamke nchini huzaa watoto watano kwa kipindi chake cha uzazi.