BurudaniUncategorized

Ripoti: Wasanii 10 wa muziki wanaotajwa kulipwa pesa nyingi kwenye show Tanzania! (Audio)

Tasnia ya muziki nchini Tanzania na Afrika Mashariki inakuwa kwa kasi zaidi licha ya kuwa inakumbwa na changamoto mbalimbali za mifumo ya kuuza kazi za wasanii hali inayosababisha wasanii wengi kushindwa kuambulia chochote kwenye kazi wanazozifanya.

Wasanii wengi wamekuwa wakitegemea zaidi shows na sio mauzo ya albamu kama ilivyokuwa hapo zamani hali iliyopelekea wengi wao kuacha kutoa albamu. Muimbaji Alikiba aliwahi kusema kwamba albamu yake ya Cinderella ambayo aliiachia mwaka 2009 ilimwingizia tsh milioni 200.

Licha ya wasanii wachache kuendelea kutoa albamu, lakini wengi wanashindwa kuachia albamu kutokana na wizi wa kazi za wasanii pamoja na kufa kwa soko la albamu baada ya wasambazaji wakubwa kama Mamu kuachana na biashara hiyo. Kwa sasa wasanii wanategemea zaidi kuingiza pesa kupitia shows pamoja na digital platform kama Mkito.Com.

Bongo5 imekuandikia list ya Wasanii 10 wa muziki wanaotajwa kulipwa pesa nyingi kwenye show hapa nchini Tanzania baada ya kufanya uchunguzi wa kina ambao umeambatana na thamani ya msanii husika pamoja na ukubwa wa muziki wake.

Hizi gharama zinaweza kuongezeka au kupungua kulingana na mazungumzo ya mteja na msanii. Pia list hii imepatikana baada ya kuzungumza na baadhi ya wasanii baada ya kuona mahitaji yao makubwa sokoni, ukubwa wao na wingi wa kazi zao ambazo zipo sokoni na zinafanya vizuri, branding zao pamoja na mambo mengine.


Diamond Platnumz.

Msanii wa muziki Diamond Platnumz ambaye ni rais wa WCB, ndiye msanii ghali zaidi kwa sasa nchini Tanzania kama ukimwitaji kwenye tukio lako lolote lazima ujipange vizuri. Kwa mujibu wa vyanzo vya ndani vinadai kwa sasa muimbaji huyo ambaye ni rais wa WCB, analipwa mpaka dola 50,000 ambayo ni sawa na tsh milioni 110 kwa show moja ya uwanjani huku zile za kawaida huwenda ikapungua mpaka dola 30,000.

 

Alikiba

Licha ya muimbaji huyo kutoka label ya RockStar40000 kupatwa na misukosuko kwenye muziki wake hivi karibuni baada ya kuachia video ya wimbo ‘Hela’ na muda mchache baadae kuufutwa YouTube baada ya kushambuliwa na mashabiki, bado ni mmoja kati ya wasanii ambao wanalipwa pesa nyingi kwa show ukiachana na Diamond. Kwa mujibu wa vyanzo vyetu vimedai muimbaji huyo kuna baadhi ya show hulipwa mpaka dola 25000 kwa shows ambayo ni sawa na tsh milioni 50 kwa show moja. Pia muimbaji huyo ni mmoja kati ya wasanii wa muziki nchini Tanzania ambao wanakubalika na mashabiki huku wengine wakimshindanisha na Diamond Platnumz.

Harmonize

Muimbaji huyu kutoka WCB ni mmoja kati ya wasanii ambao wanafanya vizuri kwa sasa kwenye tasnia ya muziki baada ya kuachia hits nyingi ndani ya mwaka. Kwa mujibu wa uongozi wake muimbaji huyo kwa sasa ili aje afanye show kwenye tamasha lako unatakiwa uwe umeandaa tsh milioni 15. Diamond aliwahi kuhojiwa na chombo kimoja cha habari na kudai project ya wimbo Iyola na Bado ziliigharimu WCB zaidi ya tsh milioni 115.



Vanessa

Huyu ni mmiliki wa label ya Mdee Music ambayo inasimamia wasanii kadhaa. Muimbaji huyo kwasasa ndiye msanii wa kike ambaye anadaiwa anaingiza mkwanja mrefu kupitia shows. Mwezi uliopita Vanessa pamoja na mpenzi wake Jux waliweza kufanya tour ya pamoja In Love & Money ambayo ilionyesha mafanikio makubwa sana. Kwa sasa ili umpate Vanessa kwenye show yake lazima uandae tsh milioni 15.


Weusi

Kundi la Weusi linalounganishwa na wasanii 5, Joh Makini, Nikki wa Pili, G.Nako, Bonta Maarifa pamoja na Lody Eyez ni moja kati ya makundi ya muziki nchini Tanzania ambayo yanafanya vizuri huwenda ni kutokana na kuwa na kazi nyingi mtaani pamoja na kila msanii kuwa na vitu vyake wakiwa stejini. Wasanii hawa ili waje kwenye show yako unatakiwa kuandaa tsh milioni 15 lakini huwenda ikapungua au kuongezeka kutokana na mazungumzo pamoja na aina ya show husika.

Rayvanny

Huyu ni msanii kutoka label ya WCB ambaye kwa sasa anafanya vizuri na wimbo Chombo, Pochi Nene na nyingine nyingi ambazo zinamfanya kwa sasa aingie kwenye list ya wasanii ambao wako kwenye mahitaji makubwa. Kwa mujibu wa taarifa tuliyopata ili muimbaji huyo afanye show unatakiwa kuandaa tsh milioni 10 mpaka milioni 15 kutokana na aina ya show na sehemu inayoenda kufanyika.

Jux

Msanii Jux ni msanii ambaye anafanya vizuri kwa muda mrefu kutokana na kutoa nyimbo kali mfululizo. Jux ambaye anamiliki brand ya nguo African Boy ili umpate kwenye show yako unatakiwa kuandaa tsh milioni 10 na hiyo inategemea na aina za show kwani inaweza kuongeza mpaka milioni 13.

Rostam

Hili ni kundi ambalo linawaunganisha wasanii wawili Stamina pamoja na Roma Mkatoliki. Wawili hawa ambao wanafanya vizuri na wimbo ‘Kaolewa’ wamekuwa wakifanya muziki nzuri ambao unawavutia mashabiki wengi kutokana na chemistry yao. Kwa sasa wawili hao ili uwapate kwenye show yako unatakiwa uandae bajeti isiyopugia tsh milioni 7 mpaka 8.


Aslay

Huyu ni msanii ambaye anamafanikio makubwa kwa sasa miongoni mwa wasanii ambao walikuwa Yamoto Band. Toka muimbaji huyo aanze kufanya kazi binafsi amekuwa ni msanii wa hit baada hit hali iliyopelekea kuwa miongoni mwa wasanii ambao wanahitajiza zaidi kwa sasa kwenye matamasha mbalimbali. Kwa sasa muimbaji huyo anafanya show kwa tsh milioni 7 lakini inaweza kuongezeka kutokana na aina ya tamasha husika.

Nandy
Huyu naye ni miongoni mwa wasanii wa kike ambao wanafanya vizuri kwa sasa nchini Tanzania kutokana na kutoa nyimbo nyingi nzuri kwa mfululizo.  Nandy pia ni mmoja kati ya wasanii wa kike ambao kazi zao kupitia mtandao wa YouTube zimeangaliwa zaidi na huwenda ndio sababu iliyofanya awe miongomi mwa wasanii ambao wanahitajika zaidi kwenye matamasha mbalimbali nchini. Kwa sasa mrembo huyo anafanya show moja kwa tsh milioni 5 lakini inaweza panda mpaka milioni 7 kutokana na aina ya show ambayo utahitaji kutoka kwake.

 

Related Articles

Back to top button

Adblock Detected

Please don't block our ads, we rely on these ads to serve you with credible contents