RIPOTI: Yanga SC yamfungulia milango mshambuliaji wake tegemezi
Kocha mkuu wa klabu ya Yanga, George Lwandamina amemruhusu mshambuliaji wake tegemezi, Matheo Anthony kuondoka klabuni hapo ili akatazame maisha sehemu nyingine baada ya kuona hatakuwa na nafasi ya kumtumia tena msimu ujao.
Matheo ambaye alijiunga na Yanga mwaka 2015 akitokea klabu ya KMKM ya Zanzibar amewekwa wazi na Kocha Lwandamina kuwa nafasi yake ya kucheza kwenye kikosi cha timu hiyo msimu ujao haitakuwepo kutokana na wingi wa washambuliaji.
Kwa mujibu wa maelezo ya mtu wa karibu wa klabu hiyo amesema Matheo ameshatuma ombi na tayari kocha na klabu ya Yanga imemkubalia kuondoka .
“Lwandamina amemruhusu Matheo kuondoka na wenzake wengine watano ambao ni Yusuf Mhilu, Baruan Akilimali, Juma Mahadhi, Maka Edward na Saidi Makapu, kocha kaona awaruhusu wote ili aweze kuangalia safu nyingine itakayokuwa na uwezo wa kutumika tofauti na ilivyosasa ambapo wengine wanaonekana kushindwa kumudu kasi yake.” kimesema chanzo hicho.
Hata hivyo imeelezwa kuwa kuna uwezekano mshambuliaji huyo akatimkia kunako klabu ya Lipuli ya Iringa au Kagera Sugar kwani tayari klabu hizo zimeonyesha nia ya kumuhitaji.