Habari

RPC Muroto azuia maandamano ya ACT ‘atakayeandamana atapigwa hadi achakae’

Kamanda wa Polisi mkoa wa Dodoma, Gilles Muroto amewatahadharisha waliopanga kufanya maandamano kesho Jumanne Aprili 9, 2019 akisema watakaoingia barabarani watapigwa na kuchakaa.

Kamanda Muroto amewaambia waandishi wa habari jijini Dodoma leo Jumatatu Aprili 8, 2019 kuwa zipo taarifa zina sambaa kwenye mitandao ya kijamii kuwa baadhi ya vyama vya upinzani ikiwepo ACT Wazalendo wamepanga kufanya maandamano kesho kushinikiza Bunge kufuta kauli yake ya kutofanya kazi na Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) Profesa Mussa Assad.

Amesema kuwa wapo wengine wamepanga kusafiri kuja Dodoma kwa ajili kufanya maandamano hayo akiwataka kuacha mara moja kwani wataambulia kupigwa na kuchakaa.

“Niwatake wale wote waliopanga kufanya maandamano kesho Aprili 9, 2019 kusitisha maandamano yao haramu, wasije kuingia barabarani maana watapigwa na kuchakaa,” amesema Muroto.

Muroto amesema kazi za Bunge zinahojiwa ndani ya Bunge na si nje ya Bunge hivyo amewataka wananchi wa Dodoma kuendelea na kazi zao kama kawaida kwani hakuna maandamano yoyote yatakayofanyika.

Hata hivyo amesema jeshi hilo limejipanga kikamilifu kukabiliana na wale wote waliopanga kufanya matukio ya uhalifu katika kipindi hiki cha kuelekea Sikukuu ya Pasaka.

Amesema askari polisi wamejipanga kuingia mtaani kuwatia mbaroni watu wa aina hiyo.

Related Articles

Back to top button

Adblock Detected

Please don't block our ads, we rely on these ads to serve you with credible contents