Habari

Serikali kutatua changamoto ya kodi shule binafsi

Serikali imeahidi kuyafanyia kazi malalamiko ya wamiliki wa shule za binafsi nchini kuhusu kodi mbalimbali wanazotozwa kwa kuwa Serikali inathamini mchango mkubwa wa taasisi binafsi za elimu katika mapambano dhidi ya adui ujinga.

Ahadi hiyo imetolewa na Naibu Waziri wa Fedha na Mipango, Dkt. Ashatu Kijaji, wakati wa sherehe za mahafali ya kumi ya kidato cha nne katika Shule ya Sekondari Baobab, iliyoko Mapinga, Wilayani Bagamoyo, mkoani Pwani.

Dkt Kijaji amesema kuwa tayari Serikali imeondoa baadhi ya kodi kwa shule hizo ikiwemo kodi ya mabango, Usalama mahali pa kazi-OSHA, Ada ya zimamoto, na kwamba kikosi kazi kilichoundwa na Serikali kupitia upya kodi zingine zinazoonekana kuwa kikwazo katika utoaji wa elimu, kinaendelea na kazi na matokeo yake yataonekana hivi karibuni.

“Niko kwenye kikosi kazi kinachoshughulikia changamoto za kodi kwenye shule za watu binafsi ninaamini suluhisho litapatikana kutokana na Serikali kuthamini mchango wenu mkubwa katika kuwapatia vijana wetu elimu,” alisema Dkt. Kijaji

Alieleza kuwa katika Bajeti Kuu ya Serikali ya mwaka 2017/2018, suala hilo litazingatiwa na kuwataka wamiliki wa shule binafsi nchini kuwa watulivu wakati jambo hilo linafanyiwakazi tena kwa umakini mkubwa.

Awali Mwanzilishi na Mkurugenzi wa Shule ya Sekondari Baobab, Bw. Halfan Swai, pamoja na kuiomba Serikali ifute kodi mbalimbali wanazotozwa kwa kuwa hawafanyibiashara bali wanaisaidia Serikali kutoa huduma kwa jamii, ameomba pia isaidie kuangalia viwango vya riba vinavyotozwa na taasisi za fedha nchini kwa kuwa zinawawekeka katika mazingira magumu wanapohitaji mikopo ya kuendeleza shule zao.

Wanafunzi 149, (wavulana 14 na wasichana 135) wa Shule hiyo wanaotarajiwa kuhitimu masomo yao ya kidato cha nne hivi karibuni, wameahidi kufanya vizuri katika mitihani yao kwa kuwa wameandaliwa vizuri na walimu waliobobea katika ufundishaji pamoja na mazingira mazuri ya kufundishia na kujifunzia shuleni hapo.

Dkt Ashatu Kijaji, mbali na kuwa mgeni rasmi katika mahafali hayo, yeye na familia yake wameshuhudia mtoto wao Samira, akiagwa wakati wa mahafali hayo yaliyohudhuriwa na watu mbalimbali wakiwemo wazazi, ndugu na jamaa wa wanafunzi hao.

Imetolewa na WFM, Pwani

Related Articles

Back to top button

Adblock Detected

Please don't block our ads, we rely on these ads to serve you with credible contents