Serikali yajibu tuhuma za ubaguzi utoaji mikopo elimu ya juu
Serikali imekanusha uwepo wa ubaguzi wa utoaji wa mikopo kwa wanafunzi wanaosoma kwenye shule za binafsi.
Hayo yamesemwa na Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, William Ole Nasha, wakati akijibu swali la nyongeza la Mbunge wa Temeke, Abdallah Mtolea(CUF) Ni vigezo vipi vinavyotumika na serikali kuwanyima mkopo wanafunzi waliosoma shule za binafsi?
“Tunachoangalia ni nani mwenye uhitaji zaidi, sio suala la kibaguzi, bajeti ni iliyopo ndogo wahitaji ni wengi. Kwa wanafunzi waliopata bahati ya kusomeshwa na wafadhili shule binafsi serikali haiwanyimi mikopo tutahitaji ushahidi kweli walifadhiliwa,” amesema Nasha
Aidha Nasha amesema kuwa, Kuhusu watoto ambao wamesoma shule binafsi kutoruhusiwa kupata mikopo ni suala la kuangalia kati ya mtu ambaye ameweza kulipa milioni 3 au 4 ya shule ya msingi na sekondari na yule ambaye hakuweza, ni yupi utampa kipaumbele kupata mkopo, sio tunabagua.