Serikali yawashukuru wananchi kufanikisha ziara ya Bush
SERIKALI imewashukuru wananchi kwa kufanikisha ziara ya Rais George Bush wa Marekani, kwa kuwa watulivu na kuonyesha mshikamano wa kitaifa wakati wote wa ziara hiyo.
Mwandishi Wa Habari Leo
SERIKALI imewashukuru wananchi kwa kufanikisha ziara ya Rais George Bush wa Marekani, kwa kuwa watulivu na kuonyesha mshikamano wa kitaifa wakati wote wa ziara hiyo.
Shukrani za serikali zimetolewa na Waziri wa Habari, Utamaduni na Michezo, George Mkuchika. Katika taarifa yake, Mkuchika aliwashukuru wananchi waliojitokeza kwa wingi kumlaki na kumuaga Rais Bush katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere Dar es Salaam.
Vile vile Serikali imepongeza vyombo vya habari nchini kwa kazi nzuri ya kuelimsha wananchi juu ya matukio muhimu wakati wa ziara hiyo.
Serikali inavishukuru vikundi vyote vya sanaa na kwaya mbalimbali vilizotumbuiza kwa umahiri uliomfanya hata Rais mwenyewe kujiunga na kucheza, amesema Mkuchika. Alisema Serikali inavipongeza vyombo vya ulinzi na usalama kwa kudumisha hali ya utulivu na usalama wakati wote wa ziara hiyo.
Ziara hii imekuwa ya manufaa makubwa kwa taifa letu. Serikali ya Rais Bush imeipatia Serikali yetu zaidi ya dola milioni 700 kwa ajili ya kuimarisha miundombinu, huduma za maji, nishati na afya, ilisema taarifa hiyo na kuongeza; Serikali inawahakikishia wananchi kuwa fedha zilizotolewa zitatumika kikamilifu kwa miradi yote kama ilivyokusudiwa, alisema.
Source: Nipashe