Habari

Shule za mihula mitatu kufutiwa usajili

Wizara ya Elimu, Sayansi, Teknolojia na Mafunzo ya Ufundi imesema itazifutia usajili shule zote binafsi, ambazo zitabainika kukiuka agizo la serikali la kuzitaka shule zote nchini kuwa na mihula miwili ya masomo badala ya mitatu, ambayo imekuwa inafuatwa na shule zisizo za serikali.

joyce-ndalichako1
Waziri wa Elimu, Sayansi, Teknolojia na Mafunzo ya Ufundi, Profesa Joyce Ndalichako

Kaimu Kamishna wa Elimu, Venance Manori alisema wizara yake ilitoa waraka huo ikiwa ni njia ya kukazia Waraka wa Serikali Namba 5 wa Mwaka 2012 ambao ulikuwa unaelekeza mihula ya masomo kwa shule za sekondari na vyuo vya ualimu, ifanane ili kuepusha usumbufu kwa walimu na kwa wanafunzi.

Waraka huo ulifafanua kuwa kila muhula utakuwa na likizo fupi na likizo ya mwisho wa muhula na siku za masomo kwa mwaka zitakuwa ni 194. Pia waraka huo unataka siku za michezo ya Umitashunta na Umiseta kwa shule za msingi na sekondari, zifanane kwa shule zote. Lakini pamoja na kuwepo waraka huo, baadhi ya shule zisizo za serikali zimeendelea kufuata mihula mitatu.

Baadhi ya shule katika ripoti za wanafunzi za mwezi Disemba kwenda kwa wazazi, wameonesha kuwa mwaka ujao wa masomo utakuwa wa mihula mitatu na nyingine minne.

“Wizara ilifanya utafiti na kujiridhisha kuwa haiwezekani shule zinazotoa elimu msingi kuwa na mihula mitatu, ndio maana tukataka nchi nzima tuwe na mfumo ambao unafanana ili kuepusha usumbufu kwa walimu na wanafunzi,” alisema Manori.

Alisema kwanza haamini kama kuna shule ambazo sio za serikali ambazo bado zinafuata mihula mitatu, na akaongeza kuwa kama zipo na wizara hiyo ikapata uthibitisho, lazima hatua za sheria zichukuliwe na hatua mojawapo ni kuzifuatia sheria.

“Ule waraka ulisambazwa kwa mamlaka zote za utekelezaji ukiwemo umoja wa shule binafsi na taasisi inayosimamia shule za dini ya Kikristo na shule za Baraza la Kiislamu, hivyo hakuna kisingizio cha mtu kutopata huo waraka, hivyo lazima wautekeleze,” alieleza Manori.

Hata hivyo, pamoja na waraka huo baadhi ya shule binafsi, zimekaidi agizo hilo na zimeendelea kufuata mihula mitatu, jambo ambalo ni kwenda kinyume cha maagizo hayo ya serikali. Kutokana na ukaidi huo, Manori alisema kuanzia mwakani, shule ambazo zitabaini kukaidi agizo hilo zitafutiliwa usajili.

Manori alisema wakaguzi wa elimu hiyo ndio kazi yao kuhakikisha kwamba maagizo yote ya serikali yanafuatwa. Pia alitoa mwito kwa wazazi ambao wanapata maelekezo ya mihula ya shule inayoenda kinyume cha maagizo ya serikali, waripoti suala hilo kwa malofisa elimu wilaya na wakaguzi wa shule.

“Sio kwamba wazazi wote waje hapa wizarani kulalamika, wale wanaoweza walete malalamiko hayo na walioko mikoani waende kwa maofisa elimu wa mikoa, wilaya na wakaguzi wa shule ili hatua stahiki ziweze kuchukuliwa,” alifafanua Kamishna huyo.

Alisema hivi karibuni wizara yake itatoa kalenda ya masomo na mihula, itakayofuatwa na shule zote zinazotoa elimu msingi, kama walivyotoa kalenda ya masomo katika mwaka huu.

Pia alikiagiza Chama cha Wamiliki wa Shule na Vyuo Binafsi nchini (TAMONGSCO), Baraza la Waislamu Tanzania (Bakwata), Tume ya Huduma za Kijamii ya Kikristo ambao ndio wanasimamia shule ambazo sio za serikali nchini, kuhakikisha wanachama wao wanatekeleza waraka huo wa serikali.

Msimamo wa Tamongsco Katibu Mkuu wa Tamongsco, Benjamin Nkonya alipoulizwa kutoa maoni yake alisema, “Niko kwenye mkutano, lakini sisi bado hatukubaliani na waraka huo wa serikali, nitumie e-mail yako nitakuandikia sababu za kupinga waraka huo.”

Hata hivyo, Nkonya baadaye alituma nakala ya barua iliyoandikwa na yeye kwenda kwa Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu, Sayansi, Teknolojia na Mafunzo ya Ufundi kumwomba shule binafsi ziendelee kutumia mihula mitatu kwa sababu inarahisisha ukusanyaji wa ada kutoka kwa wazazi na walezi.

BY: EMMY MWAIPOPO

CHANZO: HABARILEO

Related Articles

Back to top button

Adblock Detected

Please don't block our ads, we rely on these ads to serve you with credible contents