Michezo

Simba vs Nkana FC ya Mtanzania Hassan Kessy ni kesho, ‘head to head’ yawabeba miamba hiyo ya Zambia

Mabingwa watetezi wa ligi kuu soka Tanzania Bara Simba SC hapo kesho wanatarajia kushuka dimbani nchini Zambia kuwakabili wenyeji wao Nkana FC michuano ya klabu bingwa barani Afrika.

Simba SC  na Nkana FC ni timu ambazo zimepishana mwaka mmoja katika kuanzishwa kwao, mabingwa wa tetezi wa ligi kuu Tanzania wakiwa ni mwaka 1936, wenyeji wao hapo kesho wa Zambia wakiwa ni 1935.

Timu zote mbili zimepita muda mrefu pasipo kushiriki michuano mikubwa ya kimataifa na kufanikiwa kurudi rasmi mwaka 2018 kwenye ligi ya Mabingwa Afrika baada ya kushindwa kufanya hivyo kwa miaka minne tangu waliposhiriki mara ya mwisho mwaka 2014.

Katika nyanja za mafanikio Nkana FC waliwahi kufika hatua ya makundi ya Kombe la Shirikisho Afrika mwaka 2014 waliposhika nafasi ya tatu.

Rekodi ya timu hizi mbili za Nkana FC na Simba SC zinaonekana kuibeba zaidi miamba hiyo ya Zambia kutokana na kukutana mara nne huku Mnyama akipata matokeo mabaya.

Klabu hizi zitakutana kwa mara ya tano na ya sita katika mashindano ya kimataifa baada ya kufanya hivyo mwaka 1994 na 2002.

Mnamo mwaka 1994, Nkana FC na Simba SC zilikutana mara mbili kwenye hatua ya robo fainali ya Kombe la Washindi Afrika ambapo Wazambia hao waliibuka na ushindi wa jumla wa mabao 4-3.

Wakati katika mchezo uliyochezwa nchini Zambia, Nkana walishinda kwa jumla ya mabao 4-1. Wakati mchezo uliyofuata hapa Tanzania Mnyama Simba walkiibuka na ushindi wa mabao 2-0.

Kunako mwaka 2002, walikutana kwenye raundi ya kwanza ya Ligi ya Mabingwa Afrika na mchezo wa kwanza Nkana walishinda kwao mabao 4-0.

Na mchezo wa marudiano Nkana walikuja Tanzania na kupokea kichapo cha magoli 3 – 0 kutoka kwa Simba licha ya kuwa hayakutosha ili kusonga mbele kwenye hatua iliyofuata.

Wakati huo Simba ikiwa kwenye ubora wake chini ya udhamini mnono wa Azim Dewji mwaka, 1994 na hata walipokutana mwaka 2002 Mnyama alikuwa kwenye udhamini wa Mohammed Dewji ambaye ni ndugu na Azim Dewji.

Kama ilivyokuwa kwa mwaka huo wa 2002 ndivyo ilivyo sasa Simba ipo mikononi mwa muwekezaji wake Mohammed Dewji ambapo kwa sasa imeingia kwenye mfumo wa Kampuni.

Nkana FC itashuka kwenye uwanja wake wa nyumbani wenye uwezo wa kuingiza idadi ya mashabiki wanaokadiriwa 10,000 huku wakiwa sambamba na beki wao raia wa Tanzania Hassan Kessy aliyewahi kuitumikia klabu za Simba, Yanga na Mtibwa Sugar.

Miamba hiyo ya Zambia inadhaminiwa na kampuni ya uchimbaji madini ya Mopani Copper Mines wakati thamani ya kikosi chake kwa mujibu wa mtandao wa www.transfermarkt.com ni pauni 725,000 ikiwa ni zaidi ya Shilingi 2.1 bilioni.

Nkana FC ikiongozwa na baadhi ya mabeki wake kama, Hassan Kessy, Musa Mohammed, Richard Ocran, Gift Zulu, Laison Thole, Given Sinyangwe na Joseph Musonda, Ben Adama Banh hupenda zaidi soka la pasi fupi fupi ambalo husaidia kumiliki mpira na kuwasaidia katika safu yao ya ushambuliaji.

Kwenye kikao chake hii leo na waandishi wa habari mjini Kitwe kocha Mkuu wa klabu ya Simba, Kocha Patrick Aussems amesema kuwa anawafahamu Nkana  kuwa ni timu nzuri lakini amekiandaa kikosi chake vizuri ili kiweze kupata matokeo mazuri.

Related Articles

Back to top button

Adblock Detected

Please don't block our ads, we rely on these ads to serve you with credible contents