Habari

Simba wavamia zizi na kuua ng’ombe 20, Mmiliki asimulia kwa majonzi ‘Nitaanzaje maisha haya’

Kundi la wanyampori aina ya simba kutoka katika Hifadhi ya Taifa ya Serengeti (SENAPA) mkoani Mara, wamevamia zizi la mkazi wa Kijiji cha Robanda, Samwel Mahewa na kuua ng’ombe 20, huku wengine 8 wakipotea.

Tukio la kuuawa ng’ombe hao, lilitokea usiku wa Novemba 3, mwaka huu saa 7.00 usiku katika  Kitongoji cha Momorogoro kila ng’ombe mmoja akithaminishwa kuwa na thamani ya Tsh 550,000.

Akiongea na gazeti la Mtanzania, Mmiliki huyo wa ng’ombe hao, Mahewa amesema Simba walivamia zizi lake na kuua ng’ombe 17 hapo hapo na kujeruhi wengine watatu ambao walikufa baadae.

Mahewa amesema ng’ombe 8 walikimbia kutoka ndani ya zizi na mpaka sasa hawajafamika waliko, licha ya  juhudi kubwa za kuwatafuta bila mafanikio.

Alisema ndani ya zizi kulikuwa na ng’ombe ambao baadhi ni wazee na wengine walikuwa hawaoni, lakini jambo la ajabu simba hawakuwaua, bali walikuwa wanaua na kula wale walionona.

Nimepata hasara kubwa sana, Ng’ombe hawa nilikuwa nawategemea katika kilimo, Sijui nitaanzaje maisha haya,” amesema Mahewa.

Kwa upande wa Serikali, Ofisa Maliasili Wanyamapori Wilaya ya Serengeti, John ole Lendoyani alithibitisha kuuawa kwa ng’ombe hao na kumtaka Mahewa kujaza fomu ya kifuta machozi.

Ng’ombe wote waliouawa na wale waliokimbia imeelezwa kuwa na thamani yao ni Tsh milioni 15.4 .

Related Articles

Back to top button

Adblock Detected

Please don't block our ads, we rely on these ads to serve you with credible contents