Habari

Songas: Tuko tayari mkataba kupitiwa upya

Kampuni ya Songas yenye zabuni ya kuzalisha umeme wa dharura wa gesi kutoka Songosongo imesema iko tayari mkataba wake na TANESCO kupitiwa upya.

Na Gaudensia Mngumi

 
Kampuni ya Songas yenye zabuni ya kuzalisha umeme wa dharura wa gesi kutoka Songosongo imesema iko tayari mkataba wake na TANESCO kupitiwa upya.

 

Kampuni hiyo imesema itashirikiana na serikali na wadau wote wenye nia ya kuuangalia upya mkataba wao ambao Kamati ya Bunge ya Richmond iliutaja kuwa una upungufu na unawanufaisha zaidi wawekezaji na kuwaumiza wananchi wanaolipia bei kubwa ya umeme.

 

Kamati hiyo iliyoongozwa na Dk. Harrison Mwakyembe, ilipendekeza mikataba yote ya umeme ipitiwe upya ikiwemo ya Songas, IPTL na AGGREKO.

 

Mwanasheria Mkuu wa Songas, Bw. Reuben Mwaikinda, aliiambia Nipashe katika mahojiano kuwa kampuni yao haina shaka kwani imekuwa mshirika wa serikali kuzalisha umeme kwa bei nafuu na endelevu kutoka katika kisiwa cha Songo Songo kuanzia mwaka 2004.

 

Alisema wako tayari kwa wakati wote itakapohitajika kuungalia mkataba huo ambao ni wa miaka 20 unaotarajiwa kukoma mwaka 2024 na kwa sasa umefanyakazi ya uwekazaji kwa miaka minne kuanzia 2004.

 

Akizungumzia suala la `capacity charges` na gharama nyingine za uzalishaji ambazo zinalalamikiwa na Watanzania kuwa TANESCO inabebebeshwa mzigo mkubwa wa umeme unaolipwa na wateja alikubali kutaja gharama za umeme wanazozitoza TANESCO lakini hakubainisha nyingine ambazo ni mzigo kwa shirika hilo.

 

Alisema Songas huitoza TANESCO Senti za Dola za Marekani 5.5 kwa kila kilowati ya umeme kwa saa inayoiuzia.

 

Aliongeza kuwa kwa siku wanazalisha kilowati 190 za umeme wa gesi.

 

Kwa mujibu wa maelezo yake ingawa hakutaja kiasi kamili cha pesa wanazolipwa, alisema kwa kufanya mahesabu inaonekana kuwa iwapo TANESCO itanunua kilowati zote 190 za Songas italazimika kulipa Sh. 319,200 kila siku mbali na gharama nyingine za mitambo na uwekezaji.

 

Alipoulizwa iwapo TANESCO inalazimika kulipa gharama nyingine mbali na kununua umeme huo wa dharura, Bw. Mwaikinda alisema inagharamia mambo kadhaa ikiwemo mishahara ya wafanyakazi, ukarabati wa mitambo, madeni na gharama za uwekezaji. Lakini hakutaja gharama zake.

 

Alisema TANESCO pia hulipia kazi ya kuchakata gesi (gas processing) usafirishaji wake kutoka Songosongo hadi Dar es Salaam na ubadilishaji wa gesi kuwa umeme.

 

Akizungumzia gharama alisema mradi huo umewekeza Dola milioni 320 na kuongeza kuwa gharama za ununuzi wa gesi (umeme) ni kipengele kidogo katika mradi huo mkubwa wa mabilioni.

 

Alisema mambo mengine kama kujenga kituo cha umeme wa gesi, kuisafirisha na kuuingiza kwenye gridi ya umeme wa taifa ni kazi ya TANESCO.

 

Katika hatua nyingine Bw. Mwaikinda aliitetea Songas kuwa haipandishi gharama za umeme na imesaidia kunusuru wateja na bei kubwa ya nishati hiyo.

 

“Kwa kawaida jenereta zinazotumia mafuta ndizo ambazo ni ghali kupindukia,“ alisema bila kutaja IPTL ambayo huzalisha umeme wa dharura kwa njia ya mafuta.

 

Alipoulizwa kwa nini gesi izalishwe Lindi lakini umeme wake uwe ghali kupindukia, alisema tatizo si gesi kupatikana nchini isipokuwa gharama zinatokana na miundo ya kuisafirisha na kuichakata.

 

“Songas inanunua gesi kutoka Shirika la Maendeleo ya Petroli -TPDC wakati kampuni ya Pan African inaitumia kuzalisha umeme ambao unauzwa TANESCO.

 

Gharama yetu ni kuisafirisha kutoka Songosongo, kuichakata (processing) kuisafisha na kuichoma ili kupata umeme kwenye kituo cha Ubungo,“ alisema Bw. Mwaikinda.

 

Hata hivyo, hakueleza zaidi gharama nyingine za kando kando ambazo husababisha umeme huo kuwa wa bei ya juu.

 

Waziri wa Madini na Nishati aliopoulizwa juu ya utayari wa kushughulikia mikataba hasa huo wa Songas ambao wameonyesha nia ya kuupitia upya, alisema serikali imejipa muda kusubiri matokeo ya kamati ya kisekta iliyoundwa na Waziri Mkuu kushughulikia mapendekezo ya Kamati ya Bunge ya Richomnd pamoja na hoja za wabunge.

 

Hata hivyo alipoulizwa kuhusu gharama wanazolipwa kampuni ya Songas kwa siku kwa ajili ya kuendesha mitambo hiyo na mradi mzima wa gesi hakuwa tayari kutoa maelezo.

 

 

 

Source: Nipashe

Related Articles

Check Also
Close
Back to top button

Adblock Detected

Please don't block our ads, we rely on these ads to serve you with credible contents