Stars yapania ushindi
Timu ya Taifa ya Tanzania ambayo ipo kambini ikijiandaa na mashindano ya kombe la Tusker Challenge Cup inaonekana kuwa katika mazoezi makali huku baadhi ya wachezaji wakijituma kweli kweli.
Baadhi ya wachezaji wa Kilimanjaro Stars watakaoiwakilisha Tanzania Bara katika michuano ya Tusker Chalenji inayoanza mwishoni mwa mwezi huu jijini Dar es Salaam wamesifu mazoezi ya kocha wao, Jan Poulsen.
Kikosi hicho kilikuwa mapumzikoni tangu Jumatano na kinaingia kambini leo asubuhi tayari kuanza mazoezi jioni.
Kwa nyakati tofauti wachezaji wamesema kuwa mazoezi wanayopata ni mazuri na watanyesha kwa Watanzania Jumatatu watakapocheza na Harambee Stars.
”Tupo mapumzikoni, lakini mazoezi tunayofanya huko ni mazuri. Lazima kitaeleweka na hao Harambee waje,” alisema beki Stephano Mwasika.
Mshambuliaji Thomas Ulimwengu ambaye anacheza soka Sweden alisema; ”Nimejipanga vizuri na nina imani kuwa ujuzi nilioupata huko nitautumia vyema kuing’arisha timu yangu.”
”Tumejiandaa kuliko maelezo. Mimi naona Chalenji msimu huu ni nafasi yetu kuleta mabadiko na kuchukua ubingwa ambao tutautoa kama zawadi wa rais wetu,”alisema Salum Machaku, mshambuliaji wa Mtibwa Sugar.
Naye nahodha wa kikosi hicho, Shadrack Nsajigwa kwa upande wake alisema lengo ni kuiwakilisha vyema Tanzania Bara katika michuano hiyo.
”Maandalizi yetu ni mazuri kwa kweli na malengo yetu ni kuona tunaiwakilisha vyema nchi yetu,” alisema Kipa Said Mohamed anayeichezea Majimaji ya Songea na ambaye hajapata nafasi ya kuonyesha makucha yake alisema : “Tuko vizuri zaidi, wachezaji wote tupo kiushindani zaidi.”