Sumatra kuwashughulikia wanaopandisha nauli
MAMLAKA ya Udhibiti wa Usafiri wa Nchi Kavu na Majini (SUMATRA) imeomba msaada wa polisi, ili kuwadhibiti makondakta wa daladala wanaopandisha nauli kiholela
MAMLAKA ya Udhibiti wa Usafiri wa Nchi Kavu na Majini (SUMATRA) imeomba msaada wa polisi, ili kuwadhibiti makondakta wa daladala wanaopandisha nauli kiholela.
Akizungumza na waandishi wa habari mwishoni mwa wiki, Ofisa Mfawidhi wa Sumatra Kanda ya Mashariki, Walukani Luhamba, alisema tayari ameagiza askari 15 wanaotarajiwa kumaliza mafunzo Mei mwaka huu.
Luhamba alisema amewasilisha ombi lake hilo serikalini akiamini kupewa moja kwa moja askari watakaomaliza depo Moshi kwa ajili ya kazi hiyo.
Tunatarajia kupata askari 15 watakaoripoti Sumatra kwa ajili ya kazi ya kuwakamata makondakta wenye tamaa, alisema Luhamba.
Aidha, alisema hivi sasa pamoja na kupambana na wanaopandisha nauli, lakini pia wanaandaa utaratibu wa kuwakamata makondakta na kuwafikisha mahakamani kwa kosa la kupandisha nauli.
Pia Luhamba alitoa namba yake 0786 36 28 24 kwa watakaokumbana na kero kwenye daladala.
Naye Katibu Mtendaji wa Baraza la ushauri kwa watumiaji wa usafiri wa majini na nchi Kavu (SUMATRACC), Oscar Kikoyo, alisema wameandaa utaratibu wa kubandika chati za nauli katika vituo vya daladala.
Source: Tanzania Daima