Burudani

Taarifa ya kuvamiwa Tongwe Record: Waliingia wakisema ‘tunamtaka Roma na J-Murder’

Jumatano hii usiku katika mitandao ya kijamii zilianza kuzagaa taarifa za kuvamiwa kwa studio ya Tongwe Record na kukamatwa kwa rapper Roma Mkatoliki, Moni, producer wa Tongwe Record pamoja na wasanii wachanga wawili ambao majina hayo hayakupatikana mara moja pamoja na kuchua baadhi ya vifaa vya studio hiyo.

Studio hiyo ambayo iko Masaki jijini Dar es salaam ilivamiwa majira ya saa moja na nusu usiku.

Bongo5 ilifika katika eneo la tukio asubuhi ya leo na kushuhudia baadhi ya vitu ambavyo vilichukuliwa na watu hao wasiojulikana huku mwanasheria wa studio hiyo akithibitisha kukamatwa wasanii hao na kuelezea mpaka sasa hawajui wako wapi.

Hata hivyo mwanasheria huyo alisema atatoa taarifa rasmi mchana wa leo baada ya kutoa taarifa Polisi Osterbay.

Akiongea na Bongo5 asubuhi ya leo mmoja kati ya mashuhuda wa tukio hilo ambaye hakutaka jina lake litajwe, amedai watu hao walifika na gari aina ya Noah saa moja usiku na kuwakama watu 6 bila raarifa yoyote.

“Yeah ni kweli kama mlivyosikia, jana usiku studio ilivamiwa na watu wasiojulikana na hawakujitambulisha na waliwakamata watu 6, Roma, Moni,Jimmy, producer pamoja na wasanii wawili wachanga,” alisema mmoja kati ya wanafamilia ambao wanaimiliki studio hiyo.

“Walivyoingia walikuwa wakisema tunamkata Roma na J-Murder, lakini wakaondoka na watu hao na mpaka sasa hatujui wako wapi, ndo sasa hivi mwanasheria wa Tongwe Record anaelekea polisi kutoa taarifa, kwa sababu jana tulijua waachiwa muda wowote lakini mpaka sasa kimya,” aliongeza.

Taarifa zilizopo kwenye mitandao ya kijamii zinadai watu hao wamekamatwa kutokana na wimbo uitwao ‘Tanzagiza’ wa msanii ‘Sifa Digital’ ambao unadaiwa umetayarishwa Tongwe Record.

Mmoja kati ya wahusika wa studio hiyo alidai hata wao wanahisi labda hicho ndio chanzo cha tukio hilo huku wakidai wimbo huo haukutengenezwa studio hapo ila msanii huyo (Sifa Digital) aliamua kuitumia beat ya wimbo huo kinyume na makubaliano na Tongwe Record ambao ndio wamiliki wa beat hiyo ambayo tayari ilishatumika kwenye wimbo ambao alifanywa na Roma pamoja Moni.

Bongo5 ilimtafuta J-Murder ili kuzungumzia sakata hilo lakini alipokea simu na kusema kwa sasa hawezi kuongea chochote mpaka atakapopata taarifa kutoka kwa mwanasheria.

Hata hivyo katika pitapita katika mitandao ya kijamii, tulikuta taarifa ya J-Murder ambayo aliitoa Machi 27 mwaka huu kuhusu msanii huyo aliyetumia beat ya Tongwe Record.

“Sisi kama wanafamilia na uongozi mzima wa TONGWE RECORDS tunasikitishwa na kitendo cha baadhi ya wasanii kutumia midundo/ beats / instrumentals zetu za nyimbo zilizotoka kwa ajili ya kutengenezea nyimbo zao za kampeni wanazozijua wao wenyewe pasipo idhini yetu.. Tunaomba ambao washafanya hivyo wazuie kusambazwa kwa nyimbo zao hizo mara moja ili kutuepusha na lawama zitakazoletwa baada ya kufikishana kwenye vyombo vya sheria kwa kukiuka haki zetu za kikatiba. Wenu ktk ujenzi wa taifa. Junior ‘ J- Murder ‘ Makame.,” aliandika J-Murder Instagram.

Related Articles

Back to top button

Adblock Detected

Please don't block our ads, we rely on these ads to serve you with credible contents