Habari

TECNO yawakumbuka Watoto Yatima

Tukiwa katika mwanzo wa muhula wa kwanza  wa masomo, kampuni ya simu za mkononi  ya TECNO, imetoa  msaada wa vitu mbalimbali kwa watoto yatima wa kituo cha Chanika Children Shelter kilichopo Chanika Jijini Dar es Salaam ili kuwawezesha kurudi mashuleni.

Msaada huo ukiwemo wa ada kiasi cha Shilingi Milioni tatu, vifaa vya masomo, Chakula  na mahitaji mengine ya kila siku umetolewa mwishoni mwa wiki.

William Motta Meneja Masoko wa  TECNO akipeana mkono na Mkurugenzi wa kituo cha Chanika Children Shelter wakati wa kukabidhi mfano wa Hundi ya Shilingi Milioni Tatu.

Akizungumza wakati wa kutoa msaada huo Afisa Uhusiano wa kampuni ya TECNO Eric Mkomoye alisema msaada huo ni sehemu ya kuonesha ukarimu kwa watoto hao kwani jukumu la kusaidia watoto hao ni la kila mtu.

“Sisi TECNO ni sehemu ya jamii ya Kitanzania na hivyo jukumu la kuwalea watoto hawa katika kuwapatia mahitaji yao ya kila siku na kuhakikisha wanaendelea na masomo vizuri ili kutimiza ndoto zao ni letu sote” Alisema Mkomoye.

Afisa Mahusiano wa kampuni ya TECNO Eric Mkomoye akizungumza wakati wa kukabidhi msaada huo.

Kampeni ya msaada huo inayojulikana kama “Kuwa Shujaa Wangu, Kwa pamoja Tuwasaidie”, iliungwa mkono na mwanamama maarufu Esha Buheti pamoja na kampuni ya kutengeneza na kusambaza taulo za kike ya Soft Plus.

Kwa upande wake Bi Esha Buhet aliwashukuru TECNO kwa kuonesha moyo wa ukarimu na kuomba makampuni mengine yaige mfano kwa TECNO.

“Ni jambo lililonipa msukumo mkubwa sana! Nilivyoona TECNO wametoa stori  yenye simanzi ya mtoto mmoja hivi kutoka hapa, na nilisikia sio mara ya kwanza kuja wameshawahi kuja mara kadhaa, ndio maana na mimi nikaona niwaunge mkono kwa hiki kidogo nilichowaleletea, naomba na makampuni mengine yaige mfano kwa TECNO na Soft Plus”  Alisema Bi Esha.

Bi.  Esha akikabidhi baadhi ya misaada kwa watoto  wa kituo cha Chanika Children Shelter

Naye Mkurugenzi wa kituo hicho aliishukuru kampuni ya TECNO pamoja na wote walioungana kupeleka misaada mbalilmbali kwa watoto hao yatima.

“Tunashukuru  sana uongozi mzima wa TECNO pamoja na wafanyakazi wote, tunawashukuru wote mlioambatana na TECNO kuja kutupatia misaada hii. Asanteni sana” Alisema mkurugenzi wa kituo hicho.

Baadhi ya Watoto walezi wao wakiwa katika picha ya pamoja na wafanyakazi wa TECNO waliofika kukabidhi msaada.

Kituo hicho chenye zaidi ya watoto Mia moja wakike na kiume kimewahi kupelekewa msaada wa Shilingi Milioni Tano na TECNO Mwanzoni mwa mwaka 2019, pamoja na mahitaji mengine mbalimbali ya kila siku ikiwemo Chakula.

Related Articles

Back to top button

Adblock Detected

Please don't block our ads, we rely on these ads to serve you with credible contents