Habari

Treni ya kifahari zaidi duniani yawasili Tanzania na watalii 64 kutoka Ujerumani (+picha)

Watalii 64 kutoka nchini Ujerumani wamewasili Jijini Dar es Salaam leo Septemba 2, 2018 kupitia reli ya TAZARA wakitokea nchini Afrika ya Kusini kwa kutumia treni maarufu ya kitalii ijulikanayo kama ROVOS ya nchini humo.

Baadhi ya watalii kutoka Ujerumani wakifurahia burudani ya bendi ya Polisi baada ya kushuka kutoka kwenye treni ya ROVOS moja kati ya treni ya kifahari duniani, watalii hao wamekuja nchini kutembelea vivutio mbalimbali.

Watalii hao wamekuja Tanzania kwa ajili ya kutembelea maeneo mbalimbali yenye vivutio vya utalii hapa nchini ikiwemo mbuga za wanyama na visiwa vya Zanzibar.

Treni ya ROVOS iliyobeba watalii 64 wa Kijerumani kutoka Afrika ya Kusini, ikiwasili leo stesheni ya TAZARA Jijini Dar es Salaam.

Akizungumza katika hafla fupi ya kuwapokea watalii hao iliyofanyika stesheni ya TAZARA Dar es Salaam, Meneja Mkuu wa TAZARA Tanzania, Fuad Abdallah alieleza kuwa treni hiyo iliondoka mji wa Cape Town nchini Afrika ya Kusini Agosti 18, mwaka huu.

β€œWatalii mbalimbali huja nchini mara tano kwa mwaka kwa kutumia ROVOS kupitia reli ya TAZARA na nchi yetu hunufaika na ujio huu hasa faida za kiuchumi,” amesema Fuad.

Aidha alibainisha kuwa treni ya ROVOS ni miongoni mwa treni tatu bora duniani, hivyo ujio wa treni hiyo na watalii unatokana na vivutio bora vya utalii na miundombinu mizuri ya reli ya TAZARA.

Mama wa Kijerumani Linde Erdmann (katikati) akifurahia kuwasili Tanzania kwa mara ya kwanza akitokea Afrika ya Kusini kwa kutumia treni ya ROVOS kupitia reli ya TAZARA.

β€œTreni hii inatumia reli ya TAZARA kuleta watalii kwa sababu nchi yetu imekidhi vigezo vya utalii na reli yetu imekidhi vigezo vya usalama na mawasiliano ya uhakika,” aliongeza Fuad.
Alisema kuwa katika safari hiyo ya treni watalii hao pia walipata fursa ya kutembelea Hifadhi ya Taifa ya Selous iliyopo kusini mwa Tanzania na kuona wanyama mbalimbali wanaopatikana kwenye hifadhi hiyo.

Moja ya mgahawa unaopatikana katika treni ya kifahari ya ROVOS iliyowasili leo hapa nchini ikitokea Afrika ya Kusini kupitia reli ya TAZARA

Wakizungumza kwa furaha ya kuwasili Tanzania, watalii hao wa kijerumani walisema kuwa wamefurahia sana safari hiyo na mapokezi mazuri ya watanzania na kuahidi kurudi kwa mara nyingine.

Mtalii Diesknahn akizungumza na Afisa Habari wa Idara ya Habari Fatma Salum (kushoto) mara baada ya kuwasili nchini na treni ya ROVOS wakitokea Afika ya Kusini.

Kwa upande wake mfanyakazi wa treni ya ROVOS, Monica Rieder mwenye asili ya Ujerumani alisema kuwa amewahi kufika Tanzania mara 14 na anavutiwa na mabadiliko makubwa ya kimaendeleo yanayofanyika hapa nchini siku hadi siku.

ROVOS inatajwa kuwa moja ya treni tatu bora zaidi za kifahari duniani ambazo zinajihusisha na kusafirisha watalii na makao yake makuu yapo nchini Afrika Kusini.

TAZARA ni shirika la reli ya pamoja ya Tanzania na Zambia iliyoanza mwaka 1976 na inamilikiwa kwa asilimia 50 kila upande.

Related Articles

27 Comments

Back to top button

Adblock Detected

Please don't block our ads, we rely on these ads to serve you with credible contents