Tunasubiri Harusi
Mwanadada Ray C ameibuka na kusema kwamba anatarajia kuolewa na
mchumba wake Lord Eyez mwakani na habari zilizoenea mitaani ya kuwa
wameachana ni za kizushi, aliendelea kusema kwamba anafikiria kuacha
muziki na kujihusisha na biashara zake nyingine kwa madai kuwa
amechoshwa na ubabaishaji katika fani hiyo
Msanii huyo, gwiji anayesifika zaidi nchini amebainisha kuwa biashara zake binafsi zinamuingizia kipato kikubwa kuliko muziki, ambao umemjengea jina duniani.
Ray C, mwenye miaka 27 anasema mauzo ya albamu zake pamoja na wizi unaofanywa na raia unamuumiza kichwa kwa kiasi kikubwa na kumkatisha tamaa kwa vile mwaka hadi mwaka haoni mabadiliko na wadau wanazidi kunufaika zaidi kupitia yeye.
“Nikiangalia hali hii, nalazimika kufanya uamuzi mgumu ili niendelee kunufaika na maisha yangu kuliko kuishi kwa kunufaisha watu wengine,” anasema msanii huyo mwenye albamu nne sokoni.
“Nikiangalia mpaka sasa nimetoa albamu nne lakini sijapata kile nilichotegemea, naishia kukaribia jambo fulani kila mwaka bila kukipata, wakati mwingine naishia kukasirika tu. Sioni maana ndio maana nafikia hatua ya kutamani maisha wanayoishi wenzetu wa Uganda.” alimaliza kusema Ray C.