Tutatumia uwanja huu wa Kaunda- Mkwasa
Uongozi wa klabu ya Yanga umeeleza hatma ya ujenzi wa uwanja wao na kusisitiza kwamba hauna mpango wa kuhama Kaunda.
Makao Makuu ya klabu ya Yanga SC
Awali kulikuwa na taarifa za klabu hiyo kuwa na eneo Kigamboni ambako ndiko wangejenga uwanja wao, lakini Katibu Mkuu wa Yanga, Charles Mkwasa amesisitiza kwamba plani ya klabu ni kuukarabati Uwanja wa Kaunda na kuanza kuutumia na si vinginevyo.
Licha ya eneo la uwanja wa Kaunda kujaa maji kipindi cha mvua, lakini uongozi wa Yanga umesisitiza kwamba, upo katika hatua za kudhibiti maji hayo katika uwanja huo uliopo makao makuu ya klabu hiyo Jangwani, Dar es Salaam.
“Hatuna uwanja mwingine zaidi ya Kaunda na mipango iliyopo ni kuukarabati uwanja wetu huu na kuanza kutumika kama uwanja wa mazoezi,’ alisema Mkwasa na kuendelea.
“Eneo la uwanja wa Kaunda ni eneo letu kihalali na tuna kama heka 8.5, katika ukarabati wetu tutaweka uwanja wa mazoezi na maeneo mengine muhimu yanayostahili kwa mchezaji.
“Zoezi limekwishaanza kwa hatua za awali ikiwamo kuwasiliana na Nemc kuona ni vipi tutayadhibiti maji yanayotuama kipindi cha mvua.
‘Kuyadhibiti maji hayo inawezekana na kuirejesha Kaunda katika hadhi nzuri, hiyo ndiyo plani tuliyonayo katika suala zima la uwanja,” alisisitiza Mkwasa.
BY HAMZA FUMO