Kiongozi wa upinzani nchini Guinea, Cellou Dalein Diallo, amejitangaza mshindi katika uchaguzi wa urais uliofanyika Jumapili Oktoba 18, kabla ya kutangazwa kwa matokeo rasmi.
Bwana Diallo aliwaambia wanahabari na wafuasi wake kwamba ameshinda duru ya kwanza ya uchaguzi, lakini madai yake haraka yalipingwa na tume ya uchaguzi pamoja na serikali.
Hakutoa takwimu zozote lakini alisema matokeo hayo ni kwa mujibu wa chama chake, na sio hesabu rasmi ya tume ya kitaifa ya uchaguzi, ambayo bado haijachapisha matokeo. Kufuatia kauli yake hiyo, wafuasi wake walitawanyika barabarani kushangilia ushindi.
Diallo amesema kwamba vijana watatu waliuawa katika mji mkuu wa Conakry, na wengine kadhaa walijeruhiwa na vikosi vya usalama wakati walisherehekea ushindi wake.
Serikali ya Guinea pia ilisema kwamba kauli ya Diallo haikuwa ya busara kwani inaweza kuleta mkanganyiko na kutishia amani katika taifa hilo la Afrika Magharibi. Aidha serikali imesema inaweza kumfungulia Diallo mashtaka ya kosa la jinai.