Siasa

Ufisadi BoT: CCM matatani

CHAMA cha Mapinduzi (CCM) na Serikali yake vi mtegoni, na itabidi kuamua kusuka ama kunyoa kwa kuwa kuna uwezekano mkubwa kwamba fedha zilizochukuliwa kutoka Benki Kuu (BoT) chini ya Mpango wa Ununuzi Madeni (EPA), ziliingizwa katika kampeni za Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2005, uliokipa chama hicho ushindi wa kishindo, Raia Mwema imedokezwa.

Waandishi Wa Raia Mwema

 

CHAMA cha Mapinduzi (CCM) na Serikali yake vi mtegoni, na itabidi kuamua kusuka ama kunyoa kwa kuwa kuna uwezekano mkubwa kwamba fedha zilizochukuliwa kutoka Benki Kuu (BoT) chini ya Mpango wa Ununuzi Madeni (EPA), ziliingizwa katika kampeni za Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2005, uliokipa chama hicho ushindi wa kishindo, Raia Mwema imedokezwa.

 

Vyanzo mbalimbali vya habari vimeiambia Raia Mwema kwamba kiasi cha Shilingi bilioni 40 kilichochukuliwa na kampuni ya Kagoda Agricultural Limited (KAL) ili zikafanye kile kinachoelezwa kuwa ni kazi “nyeti za usalama wa nchi” sehemu yake iliingizwa katika uchaguzi.

 

Baadhi ya wabunge wa CCM waliozungumza na Raia Mwema, wamesema kwamba wana taarifa kwamba baadhi yao walipata “msaada” ili kufanikisha uchaguzi wao majimboni japo kwamba “msaada” huo ulitofautiana kati ya mbunge na mwingine, kulingana na mhusika ni nani.

 

Kwa mujibu wa wabunge hao, ambao kwa sababu za wazi hatutawataja majina, walikuwa wakipata kati ya Shilingi milioni moja hadi milioni 20, na kwamba katika matukio kadhaa baadhi yao walilalamika Makao Makuu ya chama kuhusiana na kwa nini “msaada” huo haukutolewa kwa kiasi kinacholingana kwa wote.

 

Aidha, Raia Mwema imefahamishwa kwamba kwa jinsi fedha hizo zilivyokuwa nyingi, baadhi ya wajanja ndani ya CCM waliunda mpango wa kupora sehemu yake. Kati ya matukio hayo ya uporaji lipo moja la Dar es Salaam ambako kiasi cha Shilingi milioni 600,000 taslimu zilichukuliwa lakini taarifa za wizi huo hazikufikishwa Polisi.

 

Aidha, vyanzo hivyo vya habari vinasema katika tukio jingine, mjumbe aliyetumwa apeleke fedha kiasi cha Shilingi milioni 200 Kanda ya Ziwa, badala ya kufikisha kiasi chote, aliwasilisha Shilingi milioni 80, na aliyekabidhiwa hizo 80 naye akawasilisha milioni 20.

 

Ni suala hilo, kati ya mengine, vyanzo hivyo vya habari vinasema, lililosababisha mvutano mkubwa wa uongozi hasa katika Mkoa wa Mwanza, ambako viongozi kadhaa waliwajibishwa, na wengine kuhamishwa kutokana na utata katika mgao wa fedha hizo

 

Tayari CCM, kwa kuhisi unyeti wa suala hilo, kimekanusha kuwako kwa uwezekano wa fedha hizo kuingizwa katika kampeni. Katika mahojiano na baadhi ya vyombo vya habari vilivyochapisha habari za kuhusiana na fedha hizo mwishoni mwa wiki iliyopita, vilivyowanukuu vigogo kadhaa wa chama hicho, akiwamo Katibu Mkuu, Yusuf Makamba, CCM kimesema hakikutumia fedha hizo.

 

Alisema Makamba katika mahojiano ya simu na gazeti moja wiki iliyopita: “Kwanza, siijui kabisa kampuni hiyo ya Kagoda, na chama changu huwa hakipokei fedha kutoka kwenye makampuni, zikija za Msamaria mwema kama wewe, nazipokea na ninatoa risiti. hesabu zetu ziko wazi, zimekaguliwa na juzi tu tumezipeleka kwa Msajili wa Vyama.”

 

Akijibu gazeti jingine juu ya habari hizo Makamba alisema:”Sisi tuna wanachama, ruzuku na mali zinazokifanya chama kijitosheleze. Ballali ana ofisi yake na mimi nina ofisi yangu, mlango wa kuingilia kwake siujui na wala alivyokuwa akinunua magari sifahamu.”

 

Aliendelea Makamba: “Hatuna deni lolote, wala hatuzijui hizo hela, wanaosema hivyo walizipitishia wapi? Wanaotaka kuja kutuchunguza waje wakati wowote”.

 

Alipoulizwa iwapo CCM haihusiki na mtandao uliochota fedha BoT ni kwa nini imekuwa ikihusishwa na kutajwa mara kwa mara, alijibu:

 

“Watu wanaotaja chama changu mimi sina tatizo nao, wewe mbona mke wako anakutaja taja kwani umemkosea nini?”, alihoji huku akisisitiza kuwa ofisi ya Ballali na ya CCM ni vitu viwili tofauti.

 

Alisisitiza kuwa CCM ina vyanzo vya mapato vinavyojulikana na anayetaka kujua hayo aende akachunguze ripoti ya mapato na matumizi ya chama hicho iliyokwisha kuwasilishwa kwa Msajili wa Vyama vya Siasa, John Tendwa, ya kipindi cha mwaka 2005 hadi 2007.

 

“Hesabu za CCM zimekaguliwa na ziko wazi, tunaendesha chama kwa ruzuku na tuna rasilimali za kutosha,” aliongeza Makamba.

 

Makamba, kwa mujibu wa gazeti hilo, alionyesha mshangao kwa wanaohoji matumizi ya chama hicho ambayo aliyaita kuwa “ni ya kawaida,” wakati vipo vyama, alivyodai vina matumizi makubwa lakini watu hawavihoji.

 

“Hebu niambie CCM inatumia helikopta? Lakini (Chama cha Demokrasia na Maendeleo) Chadema, wanatumia helikopta, mbona hamuwaulizi walitumia Shilingi ngapi? CCM mnaitakia nini,” alihoji.

 

Mwingine aliyezungumzia suala hilo ni Katibu wa Uenezi wa CCM, Kapteni mstaafu John Chiligati. Alisema Chiligati: “Mimi hilo silijui na wala sina taarifa nalo.”

 

Kwa upande wake, Katibu wa Uchumi na Fedha, Amos Makalla ambaye alishika nafasi hiyo Oktoba mwaka jana, akimbadili Mbunge wa Igunga na mjumbe wa Kamati Kuu ya CCM, Rostam Aziz, alisema: “Suala hilo ni uzushi unaofaa kupuuzwa. CCM ina utaratibu wa kupata mapato kupitia vitega uchumi vyake vilivyoko nchi nzima”.

 

Aliongeza Makalla: “Hao wanaodai kuwa CCM inahusika na ubadhirifu wa fedha BoT ninawashangaa sana. Watu husema kama hujafanya utafiti, huna takwimu, huna haki ya kuongea na wanaosema hivyo ni wababaishaji wanaotaka kukipaka chama matope.

 

“CCM inampongeza Rais Jakaya Kikwete kwa ujasiri aliochukua wa kuweka mambo wazi na kwamba ujasiri huo ndio ambao unawafanya wananchi waendelee kumwamini katika utendaji wake wa kazi”.

 

Mwingine aliyezungumzia suala hilo kwa mujibu wa magazeti hayo ya wiki iliyopita ni Katibu Mkuu wa zamani wa CCM, Phillip Mangula, aliyekuwa mtendaji mkuu wa chama hicho hadi mwishoni mwaka 2005.

 

“Suala hilo uongozi wa sasa unaweza kulizungumzia zaidi, lakini ninavyofahamu kwa mwaka 2005 chama kilikuwa na uwezo wa kujiendesha chenyewe bila kutegemea mtu.

 

“Tuna wanachama zaidi ya milioni 3.6 nchi nzima. Hao kama kila mmoja angechanga sh. 1000 tu unaweza kuona tungekuwa na fedha nyingi,” alisema na kuongeza:

 

“Mwaka 2005 tulijipanga na tulikuwa na kamati mbalimbali ndani ya chama kama za Uchaguzi, Fedha, Vifaa na pia kuna wanachama na mashabiki wetu walijitolea kuchangia vitu kama kofia na fulana, kwa hiyo suala la chama kujitosheleza lingewezekana kabisa,” alisema Mangula.

 

Vyanzo vya habari vilivyozungumza na Raia Mwema vinasema kwamba kujitokeza kwa vigogo hao wa CCM kuzungumzia suala lilelile, kwa wakati uleule, ni ishara kwamba hilo si jambo la kupuuza, na kama CCM haitacheza karata zake vizuri, litaibukia kuwa kashfa kubwa kwa chama hicho na Serikali kwa ujumla.

 

“Wako (CCM) katika harakati za kujaribu kufunika mambo. Wanazima moto. Na inaelekea hata nyinyi wenye vyombo vya habari mnataka suala hili liishe hivi hivi. Lakini hili si jambo la kumalizika hivyo. Mwaka 2010 kutakuwa na uchaguzi hapa. Mkiliacha yatajirudia hayahaya na huenda wengine wakachota tena BoT,” anasema mmoja wa vyanzo hivyo.

 

Vyanzo vya Habari pia vimeliambia Raia Mwema kwamba Kagoda Agriculture Company ilianzishwa kwa maelekezo ya Rais Benjamin Mkapa, na kwamba sababu za “usalama wa taifa” zilizotumiwa kuhalalisha kuchukuliwa kwa pesa hizo ndizo alizoambiwa Ballali na ndizo pia alizomwambia Meghji.

 

Aidha, nyaraka za kuuziana deni kati ya BoT na Kagoda zilisainiwa katika ofisi ya mwanasheria mmoja wa Dar es Salaam na katika kusaini huko, kulikuwa na Ofisa wa BoT na mmoja wa viongozi wa fedha katika kamati ya kampeni ya CCM.

 

Raia Mwema limeonyeshwa na mmoja wa watuhumiwa wa ufisadi huo wa BoT nakala ya hundi ya malipo kwa Katibu Mkuu wa CCM.

 

Habari zaidi zinasema pia kwamba kampeni za uchaguzi wa mwaka huo zilikuwa zikiendeshwa nje ya ofisi ya makao makuu ya CCM, na hivyo kumfanya aliyekuwa Katibu Mkuu, Mangula asijue kila kitu kilichokuwa kikiendelea.

 

“Kampeni ziliendeshwa katika ofisi binafsi ya mmoja wa wajumbe wa sasa wa Kamati Kuu ya CCM na huko ndiko fedha zote za kampeni zilipelekwa, na hivyo CCM kutaka kujiaminisha kuwa haihusiki na fedha chafu ni kujaribu kuficha ukweli,” kilisema chanzo hicho cha habari.

 

“Fedha zilizochotwa BoT na Kampuni ya Kagoda zililipwa kupitia benki moja ya ndani na hii inarahisisha sana kazi ya uchunguzi kwani ni rahisi sana kujua ni nani alikwenda kuchukua fedha hizo Benki,” kilisema chanzo hicho cha Habari.

 

Aidha baadhi ya watu ndani ya vyombo vya dola waliohojiwa na gazeti hili wanasema, kama kweli Serikali ina nia ya dhati kushughulikia wahusika, kamati inayoongozwa na Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Johnson Mwanyika, haipaswi kusubiri kufikisha kundi la watuhumiwa mahakamani na badala yake kufikisha wale ambao ushahidi wa jinai dhidi yao uko wazi kabisa kama ule wa Kagoda.

 

Katikati ya sakata hili la BoT ni Dk. Daudi Ballali – Gavana wa zamani wa BoT aliyetimuliwa kazi hivi karibuni na Rais Kikwete. Dk. Ballali, ambaye amekuwa akijiuguza nchini Marekani, ndiye anayeonekana kutwishwa mzigo wote wa ubadhirifu ndani ya benki hiyo mhimili wa uchumi wa Tanzania.

 

Taarifa za karibu na yeye zilizoifikia Raia Mwema, zinasema amekuwa akishangazwa na jinsi ambavyo vigogo wanavyojitahidi kumgandamiza katika suala hilo.

 

“Bado anaumwa. Anahisi kuwa ugonjwa wake, pamoja na sababu nyingine, umetokana na sumu, walau madaktari bingwa wa Marekani anakotibiwa wamemwambia kuwa alikula sumu. Kwa hiyo amefanyiwa operesheni ya tumbo. Haijulikani itachukua muda gani kupona, na ndiyo maana aliandika barua ambayo haikujibiwa ya kujiuzulu. Lakini Mungu si Athumani. Akijalia Mwenyezi atapona. Akipona, kama ambavyo wote tunaomba kwa Mungu, atakuja kuzungumza.

 

“Ana kila ushahidi. Ana kila aina ya nyaraka zilizokuwa zikimtaka afanye nini. Hakika akifanikiwa kuzungumza watu wataumbuka. Si kuwa yeye ni malaika, lakini madhambi mengi wanataka kumbebesha yeye,” alisema.

 

“Na hicho ndicho vigogo nchini wanachokiogopa. Akiweza kusema tutashangaa, na tutawashangaa viongozi wetu. Hivyo ili asiweze kusema ndiyo kila mara unasikia mara kafukuzwa kazi, mara visa yake imetenguliwa na mara anakaribia kufa.

 

“Wanataka afe ili siri isifichuke. Kuna uongo mwingi. Na mwenye ufunguo wa uongo huo ni yeye. Anajua na hata baadhi ya wafanyakazi wa BoT wanajua nani alikuwa akishinda ofisini kwake, kwa mfano, kushinikiza malipo ya kampuni ya Kagoda.”

 

Ndugu huyo wa karibu wa Dk. Ballali amesema Gavana huyo aliyepita wa BoT anataka afikishwe Mahakamani ili ukweli wa nani alishiriki vipi uweze kuanikwa huko.

 

“Ametuambia kwamba anataka sana kwenda Mahakamani. Huko anatarajia jina lake litasafishwa. Na wanaombeza leo nao sheria ichukue mkondo wake juu yao,” anasema ndugu huyo wa Dk. Ballali ambaye anazungumza naye mara kwa mara.

 

Baadhi ya wakongwe katika fani ya sheria wanasema endapo kweli Serikali italifikisha suala hilo Mahakamani, itasaidia kuibua mambo mengi ambayo pengine yakafungua ukurasa mpya wa demokrasia na utawala bora.

 

 

 

Source: Raia Mwema

Related Articles

Check Also
Close
Back to top button

Adblock Detected

Please don't block our ads, we rely on these ads to serve you with credible contents