Ufisadi umetuweka pagumu – Pinda

Waziri Mkuu Mizengo PindaWaziri Mkuu Mizengo Pinda amesema kwamba kuibuliwa kwa masuala ya rushwa kwa viongozi wa serikali kulikofanywa na vyombo vya habari, kumeiweka serikali mahali pagumu, na kwamba sasa watendaji wake inabidi wawe makini zaidi

Mgaya Kingoba


 


Waziri Mkuu Mizengo Pinda amesema kwamba kuibuliwa kwa masuala ya rushwa kwa viongozi wa serikali kulikofanywa na vyombo vya habari, kumeiweka serikali mahali pagumu, na kwamba sasa watendaji wake inabidi wawe makini zaidi.

Akizungumza na wahariri wa vyombo mbalimbali vya habari Dar es Salaam jana, Waziri Mkuu alisema kuibuliwa kwa masuala hayo ya rushwa kwa viongozi na kulazimisha wengine kujiuzulu, ni changamoto kubwa na sasa inabidi mawaziri wawe makini na waangalifu zaidi.

“Hapa mlipotufikisha sasa ni pagumu,” alisema Pinda na kuongeza kuwa ingawa masuala mengi ya vitendo vya rushwa yalifanyika katika awamu zilizopita, lakini ni changamoto kwa serikali ya sasa kujitahidi kuhakikisha haiangukii katika mtego wa wengine kutuhumiwa kushiriki vitendo hivyo.

“Hii imetufanya tuwe makini zaidi, (wanahabari) mmesukuma sana mambo. Mmefanya kazi nzuri na mnapaswa kuendelea kufanya kazi hiyo na ni juu yetu sisi kuhakikisha hatuingii katika mtego. Awamu hii inatakiwa tuwe waadilifu sana, ili hata kama itakapomalizika miaka mitatu minne, isije ikasemwa tena Mzee Pinda nawe ulichukua,” alisema Waziri Mkuu.

Alivipongeza vyombo vya habari kwa kazi nzuri ya kufichua ufisadi, akisema yeye anaunga mkono kazi hiyo na kwamba muhimu ni kuhakikisha vyombo hivyo vinaandika habari za kweli bila kupotosha na pia kujali maslahi ya Taifa.

Akijibu maswali ya wahariri hao kuhusu masuala mbalimbali, Waziri Mkuu alirudia kauli yake aliyoitoa bungeni mwezi uliopita kuwa wahusika wa kashfa ya Richmond watachukuliwa hatua kama ambavyo wamependekeza wabunge, lakini hilo litakwenda hatua kwa hatua.

Mojawapo ya hatua hizo ni suala la uingiaji wa mikataba ambalo alisema linaonyesha Watanzania hawana ujuzi nalo, na akapendekeza katika mchakato wa kusaini mikataba, kuwe na kamati huru ya wataalamu binafsi itakayopitia na kutoa mapendekezo kabla ya mikataba kusainiwa.

Alipinga wazo la mikataba hiyo kupelekwa kwanza bungeni, akisema chombo hicho cha kutunga sheria kitapoteza jukumu lake la msingi na kujiingiza katika matatizo. “Hatujalala, ila hatuwezi kukamata watu; kuwaweka ndani na kuchukua mali zao kama baadhi ya watu wanavyopendekeza.

Hakuna anayetaka kukumbatia uovu, lakini zaidi tufuate taratibu,” alisema Pinda.
Alikiri kuwa mkataba wa Kitengo cha Kuhudumia Makontena Bandari (TICTS) ulikuwa na walakini na kwamba serikali inafanya taratibu za kuhakikisha mkataba huo unapitiwa upya na kusema; “Nadhani la TICTS tutalimaliza.”

Kuhusu wanasiasa wanaotuhumiwa kwa rushwa na ufisadi kupokewa kwa sherehe kubwa wanaporudi maeneo wanayotoka, Waziri Mkuu alisema hilo ni la mtazamo wa watu zaidi hasa wale wanaompokea.

Kuhusu kauli yake ya kutaka mafisadi hao watenganishwe na vyama, alisisitiza kwamba si vyema wakahusishwa na chama au serikali kwa sababu siyo sera ya chama wala serikali kuhusu rushwa na ufisadi, bali matatizo hayo yanatokana na hulka na tamaa ya mtu binafsi. “Chonde, chonde, ufisadi siyo sera ya chama wala serikali; chama na serikali vinakemea hili.

Mtu mmoja kwa sababu ya ulafi wake, tamaa zake, tukimpata jukumu ni moja; kumfuatilia achunguzwe na kisha sheria za nchi zichukue utaratibu wake,” alisema Waziri Mkuu. Alipoulizwa anajisikiaje kuhusu madai kwamba wapo baadhi ya watu waliokamatwa kwa kumzomea Rais mstaafu Benjamin Mkapa kwa madai ya kuhujumu uchumi, Waziri Mkuu alijibu;

“Ninachoogopa ni kuanza kuhukumu watu, siyo nzuri, si sahihi. Kuchukua sheria mkononi si sahihi.” “Mimi siafiki hata angekuwa mtu mwingine yeyote. Huyu ana heshima yake, ni binadamu. Ana haki yake kama Mtanzania, ana mahali pake apelekwe huko. Zipo taratibu za kufuatwa, lakini siyo kuzomea,” alisema Waziri Mkuu katika mkutano huo uliodumu kwa zaidi ya saa mbili.

Alipoulizwa kuhusu mikakati inayochukuliwa kupunguza mapigano ya wenyewe kwa wenyewe mkoani Mara, Waziri Mkuu alikiri kuwa Mkoa wa Mara una matatizo yanayotokana na utamaduni na hulka za wenyeji wa mkoa huo, lakini akapendekeza kuwa wataalamu wa sosholojia wapelekwe kufanya utafiti na kubaini jinsi serikali inaweza kutatua matatizo hayo.


 


Source: Habari Leo

Related Articles

Check Also
Close
Back to top button

Adblock Detected

Please don't block our ads, we rely on these ads to serve you with credible contents