Urais TFF: Marcio Maximo ampigia upatu ‘mhenga’ mwenzake (Video)
Aliyekuwa kocha mkuu wa timu ya taifa ya Tanzania (Taifa Stars ) raia wa Brazil, Marcio Maximo amempigia upatu mgombea nafasi ya urais wa Shirikisho la Mpira wa Miguu nchini (TFF), Frederick Mwakalebela kuwa ana stahili kukabidhiwa nyadhifa hiyo kwakuwa ni muumini wa soka la vijana.
Marcio Maximo amesema kuwa “Kwanza kabla ya yote ningependa kusema kwamba wagombea wote wa TFF ni wazuri na wanavigezo vya kuwania nafasi ya urais”.
Maximo ameongeza “Lakini ningependa kusema kwamba kwa nini namsapoti, Mwakalebela nadhani ni rahisi tu yeye amewahi kufanya kazi na mimi katika kipindi cha uongozi wa Tenga ambaye alikuwa rais mzuri wa shirikisho hilo naamini anaweza kufuata nyayo zake, lakini pia yeye ni muumini wa soka la vijana, soka la wanawake pia naamini TFF hawatafanya makosa kama walivyofanya katika wakati wangu”, amesema Marcio Maximo.
Taifa Stars ilikuwa chini ya Kocha mrazili, Marcio Maximo kuanzia mwaka 2006 ambapo aliiwezesha kushiriki michuano ya CHAN mwaka 2009.
Miongoni mwa mambo ambayo alifanikiwa kocha huyu ni Kurudisha ari, moyo na uzalendo kwa wachezaji, mashabiki na wadau wa michezo nchini kiasi ambacho watu wengi walihudhuria wakati Stars ikiwa inacheza na hata kununua jezi zake .
Maximo aliiongoza Stars kuanzia mwaka 2006 hadi 2010 na katika kipindi hicho ikifanikiwa kucheza michezo 43 na kushinda michezo 16, ikitoka sare 15 na kufungwa mechi 12.
Pia alifanikiwa kufanya mapinduzi ya soka la Tanzania baada ya kuipandisha Stars hadi nafasi ya 108 katika viwango vya soka vya dunia vinavyotolewa na FIFA.
Mgombea wa nafasi ya urais wa TFF, Frederick Mwakalebela ambaye anaonekana kuwa chaguo la Maximo yupo katika mbio za kuwania nafasi hiyo huku miongoni mwa vipaumbele vyake ikiwa ni kusimamia utawala bora kwa kufuata katiba na sheria ili kuendesha vyema mpira wa miguu huku akiahidi kusimamia timu ya Taifa kwa kupanga mkakati maalumu utakaoweza kusaidia mchezo wa mpira wa miguu nchini
Miongoni mwa mambo mengine ambayo ameahidi kuyatekeleza endapo atapata nafasi hiyo ni pamoja na kuhakikisha vyama shiriki na vyama vya mikoa vinakuwa na vitendea kazi na kuwa na ofisi za kudumu katika kuhakikisha unarahisisha kazi.
By Hamza Fumo