Urusi na Ukraine wanataka kuwepo na usitishwaji kabisa wa mapigano mashariki mwa Ukraine ifikiapo mwishoni mwa mwaka huu wa 2019.
Rais wa Ukraine Volodymyr Zelensky (kushoto) na Vladimir Putin (kulia)
Haya yamebainika mjini Paris, Ufaransa katika mkutano wa kilele uliofanywa kama ule wa Normandy. Rais wa Urusi Vladimir Putin na mwenzake wa Ukraine Volodymyr Zelensky mbali na mambo mengine wamekubaliana pia kuondoa vikosi katika eneo la mpakani na kubadilishana wafungwa.
Kwa mujibu wa chombo cha habari cha DW, Mkutano huu wa kilele uliowapatanisha kwa mara ya kwanza Putin na Zelensky umeandaliwa na Kansela wa Ujerumani Angela Merkel na Rais wa Ufaransa Emmanuel Macron.
Nchi hizo mbili pamoja na viongozi wake wanataka kuwa na maelewano katika kipindi cha miezi minne ijayo.