Bongo Movie

Utajiri wa mashaka wa wasanii wa kike wa filamu nchini

Wiki iliyopita katika kipindi cha Take One cha Clouds TV, watu hawakuamini kile walichokiona, kinachodaiwa kumilikiwa na muigizaji maarufu wa filamu nchini, Wema Sepetu. Ni nyumba ya kifahari iliyopo Mikocheni jijini Dar es Salaam ambayo kwa wale walioiona walipatwa na maswali mengi, lakini moja kubwa, ni Je! Tasnia ya filamu nchini Tanzania inalipa kiasi cha kufanya waigizaji kama Wema waishi maisha kama ya Hollywood?
Katika kipindi hicho Wema alichukua muda mrefu kuwazungusha waandaaji wa kipindi hicho ambapo camera zilikuwa na uchu wa kumulika vitu vilivyomo kwenye mjengo wa kifahari wa Miss Tanzania huyu wa zamani. Kama kilivyo kipindi maarufu cha MTV Cribs, Wema alizunguka kila kona ya nyumba yake kuwaelezea kile alichoweza kuelezea.
Alifungua kabati za chumbani na pia aliwapeleka sebuleni kuona jinsi sebule ilivyoshona vitu vya kifahari ambavyo mara nyingi watanzania wa kawaida huishia kuviona kwenye filamu tu. Aliwapeleka bafuni kujionea majakuzi ya kufa mtu ambayo bei zake yaweza kuwa ada za wanafunzi zaidi ya watatu chuo kikuu. Camera za kipindi hicho zilimulika kila kona ya nyumba hiyo ambayo kwa haraka haraka Wema anasema imemgharimu kama milioni 400 hivi! Haswaa shilingi milioni 400 na hatujakosea.

Ni fedha ambazo anasema zimetoka mfukoni mwake mwenyewe! Basi ilikuwa raha tupu! Kwa wanaoidharau tasnia ya filamu nchini wakasema alaaa! Kumbe hawa watoto wana hela hivi! Kuanzia hapo kila mmoja akampa salute Wema, kwamba mtoto hela anayo. Nani asiyetaka maisha yale? Wakati kipindi kinaendelea wakaibuka watu weeengi waliokuwa na mashaka na habari hiyo. Wema wanayemfahamu kapata wapi hela zote hizo? Sawa, wanakubali kuwa pesa anayo kutokana na mishemishe zake, lakini ndo zote hizo kweli?
Wakati akielezea kwa bashasha kabati lililopo chumbani mwake na kudai kuwa anaishi mwenyewe kwenye mjengo huo isipokuwa wafanyakazi wa ndani kadhaa, mtangazaji wa Clouds FM Barbara Hassan akatweet ujumbe unaosema ameona nguo za kiume kwenye kabati, iweje Wema aseme yupo single na anaishi mwenyewe kwenye nyumba hiyo? Wengi story hii haikuwaingia akilini. Wakasubiri kuona kama kuna ukweli mwingine utaibuka baadaye kutoka kwenye story. Usemi usemao ‘Lisemwalo lipo kama halipo laja,’ jana (June 18) ukajidhihirisha! Kwa mujibu wa mtandao wa Teentz, mmiliki halali wa nyumba hiyo ameibuka ikiwa ni siku chache tu tangu mrembo huyo ajinadi kwenye TV kwa show kama ya MTV Cribs! Mtandao huo umesema mmoja wa watu walio karibu na mmiliki huyo mwenye asili ya kiarabu aitwae Ahmed au Msafiri jina linalojulikana zaidi mitaa yake, amesema kuwa Wema aliutangazia umma juu ya umiliki wake kwa nyumba hiyo wakati ambao kijana huyo wa kiarabu alikuwa safarini nchini Brazil kwenye michongo yake. Umemnukuu akisema, “Unajua Wema amewadanganya watu kwa kiasi kikubwa, nafikiri anatakiwa kuomba radhi nakuwaeleza ukweli kwenye nyumba ile hana hata kipande cha tofali na mmiliki halisi ni mshikaji wangu Ahmed ambaye mara kadhaa huwa anasafiri kwenda nchini Brazil kibiashara.” Kama habari hii ni ya kweli, ni ngumu kupata jibu la lengo la Wema Sepetu kuchukua muda wa watu wanaoangalia TV kuwadanganya anamiliki nyumba ambayo hajatoa hata senti katika kuijenga. Tukisema anatafuta umaarufu tunakuwa hatujapata sentensi sahihi kuelezea dhamira yake kwakuwa Wema ni maarufu nchini kama ilivyo bangi kwa rastafarai. Lengo lake lilikuwa nini? Kwanini atafute publicity kwa kuudanganya umma? Hitimisho la mkasa huu kwenye akili za watu wengi ni moja na rahisi kabisa. Kwamba Ahmed ni mpenzi wake na Wema. Amejenga nyumba na kumkabidhi Wema aishi kwakuwa yeye ni mtu mishe mishe! Japo safari zake za Brazil kwa mujibu wa mtu wake wa karibu zinatupa mashaka kutokana na utajiri alionao kwa kujenga nyumba hiyo na historia ya Brazil katika upatikaji wa kile unachokifiria sasa kichwani mwako, si suala letu hapa. Suala ni kwanini Wema anadanganya?
Wema Sepetu ni mmoja tu kati ya waigizaji kadhaa wa Bongo Movies wanaotiwa mashaka kutokana na utajiri wao. Bahati nzuri ni kuwa majibu ya utajiri wao yanaanza kuja pole pole kuwa, unatokana na kuhongwa na wanaume! Kwenye orodha hiyo jina linaloanza kuzunguka kwenye akili yako wewe unayesoma makala hii bila shaka ni Jackline Wolper. Hivi karibuni ameandikwa sana kwenye mtandao na magazeti ya udaku kuhusiana na utajiri wake. Wengine walifikia hatua ya kusema utajiri huo huenda unatokana na kujiunga na Freemason. Kama ulivyo msimamo wa Bongo5 juu ya uhusiano wa dhana hiyo na utajiri wa baadhi ya wasanii nchini, ni ujinga kufikiria kuwa hiyo inaweza kuwa sababu. Jackiline aliwashangaza watu baada ya kubainika kuwa pamoja na mengine, anamiliki mkoko aina ya BMW X6 wenye thamani ya shilingi milioni 170.
Wengi walikuwa na jibu tayari kuwa magari hayo yanatokana na kuhongwa ila walikuwa wakisubiri tu kupata jibu sahihi. Mtandao wa Dartalk uliwahi kufanya uchunguzi na kugundua kuwa mbwembwe za magari hayo ya kifahari zinatokana na kuhongwa na mtu mmoja mzito sana kwenye benki maarufu nchini japo yeye alikanusha. Kama Bahati tu, umetokea mgongano kuwa mtandao huo huo wa Teentz umezikamata za chini ya carpert kuwa jamaa huyo amemnyang’anya gari hilo Jackline baada ya kugundua kuwa licha ya kupewa good times na bosi huyo, Jackline alikuwa anagawa uroda kwa bishoo mmoja anayemiliki duka la nguo mitaa ya Kinondoni (zile za mafiga matatu, si unajua).
Japo ni vigumu kuthibitisha habari hizo kwa sasa, mtandao huo umesema sasa hivi muigizaji huyo amekuwa akiendesha gari aina ya Noah ambalo kwa mujibu wa habari za mwanzo ni kwamba gari hilo alilitumia kwa ajili ya kuwapeleka shule na kuwarudisha nyumbani wadogo zake. Story za waigizaji hao wawili zinajibu maswali ya wengi kuhusiana na utajiri wa baadhi ya wasanii wa filamu nchini. Hata hivyo ni wazi kuwa waigizaji wengi waliopo kwenye biashara ya filamu hujikuta wakisakwa na wanaume wengi ambao lengo lao ni kuwafaidi tu na kutimiza haja zao. Uamuzi wa kukataa ama kukubali kugeuka vyombo vya starehe na kuchafuliwa majina yao kwenye jamii unabaki mikononi mwao.
Hii ni dunia huru kabisa.

Related Articles

Check Also
Close
Back to top button

Adblock Detected

Please don't block our ads, we rely on these ads to serve you with credible contents