Video: CUF upande wa Lipumba waomba radhi wapiga kura wao
Chama cha Wananchi(CUF), upande wa Profesa Ibrahim Lipumba anayetambuliwa na Msajili wa Vyama vya siasa nchini wamewaomba radhi wapiga kura wa jimbo la Kinondoni baada ya aliyekuwa mbunge wa jimbo hilo kupitia chama hicho, Maulid Mtulia kujiuzulu kwa kile alichodai anaunga mkono juhudi za Rais Magufuli.
Akizungumza na waandishi wa habari leo Makao Makuu ya chama hicho Buguruni, Mkurugenzi wa Habari, Uenezi na Mawasiliano ya Umma, Abdul Kambaya amesema Chama hicho hakikutarajia kuingia katika uchaguzi mdogo hasa jimbo la Kinondoni kabla ya Uchaguzi Mkuu.
“CUF haikutarajia kuingia katika uchaguzi mdogo hasa jimbo la Kinondoni kabla ya Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2020 labda kingetokea kifo. Tunawaomba radhi wakazi wa Kinondoni,” amesema Kambaya.
Aidha amesema kuwa CUF iliwaaminisha wakazi wa Kinondoni kwa kumpeleka Mtulia kugombea jimbo hilo kwa kuwa ni mtu makini.
Disemba 2 mwaka huu, Mtulia alitangaza kujiuzulu nafasi ya zot za uongozi ndani ya chama hicho na kujivua uanachama.