Burudani

Video: Hotuba ya TID ni mwanga mpya wa maisha yake

Msanii wa muziki wa Bongo Fleva Khalid Mohammed maarufu kama TID, Jumatatu hii amekiri kuwa amekuwa akitumia madawa ya kulevya mbele ya mkuu wa mkoa wa Dar es Salaam na viongozi wengeni huku akitazamwa na wananchi kupitia runinga zao.

Hatua hiyo imekuja baada ya wiki chache zilizopita kuwa miongoni mwa wasanii waliotajwa na Mhe. Makonda katika orodha ya kwanza ya majina ya watu wanaojihusisha kutumia dawa hizo haramu zinazopigwa marufuku dunia nzima.

TID ni mmoja kati ya mfano bora na wa kuigwa na watu wengine kutokana na kile ambacho amekisema bila ya kuficha jambo lolote tena mbele ya hadhara. Hakika nimefurahia kwa uamuzi aliouchukuwa msanii huyu hasa hotuba yake aliyoitoa Jumatatu hii katika ukumbi wa JNICC mbele ya viongozi mbalimbali wakiongozwa na Makonda imeonyesha ni jinsi gani alivyoamua kutoka kwa miguu yote kwenye giza hilo nene.

Ni watu wachache ambao wanaweza kusimama mbele ya watu wengi huku dunia nzima ikiwa inakuangalia kupitia vyombo mbalimbali vya habari na kutamka maneno ya busara na hekima pamoja na kukiri kosa kwa kuomba radhi watu wote wakiwemo mashabiki wake kwenye muziki huku akidhihirisha kuwa anamshukuru Makonda kwa kile alichokifanya maana ndio umeonekana ulikuwa kama uokozi wake kwenye janga hilo na kuwaacha midomo wazi wengi waliodhania kuwa atajenga chuki na kiongozi huyo wa mkoa.

Baadhi ya maneno yaliyowafurahisha wengi kutoka kwenye hotuba yake ni pamoja na kusema, “Nimesimama hapa kama kijana shupavu, mpambanaji , mwenye nguvu mpya lakini nipo hapa mbele yenu kama mnyama. Nipo tayari kuiunga mkono vita hii ya madawa ya kulevya, narudia tena mnyama mkubwa. Maana vita hii inabidi uwe mnyama kama kaka yangu Makonda ili uweze kushinda, napenda kutoa shukrani zangu za dhati kwa kaka yangu Makonda.”

“Wengi wamejiuliza imekuwaje na kwanini? Hakuna anayejua nimepitia mangapi hadi kufika hapa, lazima nilihitaji nguvu ya dola. Sometimes in life you can mess it up, you can try again. Mimi nashangaa watu wengine wanasema yule jamaa sasa ndio atakuwa snitch. What should I do? Nikae niendelee kuwa muathirika au nipate msaada.”

“This is a public disaster. I want to be good example for my life na society nzima. Imagine mtoto wangu Jamal sasa hivi aone anafuata nyendo za baba yake nitakuwa mimi sanaa ya Tanzania au Tanzania kwa ujumla nimeifanyia nini?,” ameongeza TID kwenye hotuba hiyo.

Huu ni wakati wa kumpongeza msanii huyu kwa ujasiri huo lakini pia tunatakiwa kumuombea zaidi ili stori isije kubadilika tena akarudi kwenye bahari ya janga hilo yenye mawimbi mazito kwani hotuba yake aliyoitoa inaingia katika historia ya vichwa vya wengi na kuwa historia ya mwanga mpya wa maisha yake.

Related Articles

Back to top button

Adblock Detected

Please don't block our ads, we rely on these ads to serve you with credible contents