‘Wafanyakazi wa Hotel ya 77 Arusha hawatudai’ – Serikali
Wizara ya Fedha na Mipango imesema kuwa waliokuwa wafanyakazi wa Hoteli ya Seventy Seven ya mkoani Arusha, walioachishwa kazi mwaka 2000, wameshalipwa mafao yao kwa mujibu wa sheria na taratibu hivyo hawastahili kudai malipo yoyote ya nyongeza.
Naibu Waziri wa Fedha na Mipango (MB), Dkt Ashatu Kijaji, ameyaeleza hayo bungeni mjini Dodoma, alipokuwa akijibu swali la msingi la Mbunge wa Viti Maaluum (CCM) Arusha, Mhe. Catherine Magige aliyehoji,
Je?, “ni lini Serikali itawalipa mafao waliokuwa wafanyakazi wa hoteli hiyo huku akiliambia bunge kuwa waliokuwa wafanyakazi wa hoteli hiyo ambao waliachishwa kazi mwaka 2000, hawajalipwa mafao yao hadi sasa.
Akijibu swali hilo, Dkt. Kijaji alisema kuwa Waliokuwa wafanyakazi wa hotel ya Seventy Seven Arusha wapatao 238 waliachishwa kazi mwaka 200 na kulipwa mafao yao kwa mujibu wa taratibu na sheria katika zoezi la uliwaji wa mafao hayo serikali kupitia iliyokuwa PSRC ilitoa na kulipa kiasi cha shilingi 217,366,296 mwezi Januari, 2000 kama mafao ya wafanyakazi hao.”
Alifafanua “Baada ya malipo hayo wafanyakazi waliwasilisha malalamiko kuwa wamepunjwa PSRC ilihakiki madai hayo na baada ya kujiridhisha mwezi Agosti mwaka huo wa 2000 serikali ilitoa idhini tena ya kulipa tena kiasi cha shilingi 273, 816, 703 kugharamia mapunjo ya mshahara na mafao ya wafanyakazi hao. Hivyo basi wafanya kazi hao tayari walishalipwa mafao yao kwa mujibu wa sheria na taratibu na hawastahili kudai malipo yoyote ya nyongeza.”
Na Emmy Mwaipopo