Habari

Wakati huu ni wakujituma wenyewe – Makamu wa Rais

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan amewaambia watendaji kuwa huu si wakati wa kuambiwa kufanya kazi ni wakati wa kujituma mwenyewe.

Makamu wa Rais aliyasema haya wakati akihutubia wakazi wa Iringa mjini kwenye mkutano wa hadhara uliofanyika kwenye viwanja vya Mwembetogwa.

“Naomba sana watendaji tubadilike tutoke maofisini tuone kinachotokea tumezoea kukaa maofisini, wakati huu ni wakati wa kujituma wenyewe.”

“Sijaridhika na jinsi wananchi wanavyofanya shughuli zako kule kwenye vyanzo vya maji, sijaridhika na namna waheshimiwa wabunge na viongozi wengine wanavyolinda wananchi wanaoharibu vyanzo vya maji na hili nimesema niliseme hapa tupo sote, kwenye vyanzo vya maji hakuna mbadala, hakuna mswalie mtume tunapodai tupate maji safi na salama haya maji hatutengenezi sisi serikali kuu haya maji yanatoka kwenye vyanzo vyanzo ambavyo vinataka vitunzwe,” alisema.

Makamu wa Rais aliwataka Viongozi kusimamia haki za wanyonge na kuhakikisha haki inatendeka kwa wanyonge ambao wengi wamedhulumiwa mali hasa ardhi.

Makamu wa Rais aliwataka wananchi kuzidai halmashauri zipeleke pesa kwenye miradi ya maendeleo ,pia alizitaka Halmashauri kuzisimamia zile pesa asilimia 10% kwa ajili ya Wanawake na Vijana zinatoka lakini pia kusimamia zinavyotumika.

Makamu wa Rais aliwaasa wakazi wa Iringa mjini kuwa makini na Viongozi ambao hawapendi maendeleo kwa kuwazuia kushiriki kwenye miradi ya maendeleo, aliwaambia wananchi hao maendeleo hayana chama.

Makamu wa Rais aliwaagiza uongozi wa mkoa kuanza kurasimisha biashara zisivyo rasmi kwa kuanza kuwatambua wamachinga, kuwasajili na kuwapa vitambulisho na kuwaunganisha kwenye mifuko ya jamii na bima ya afya pia kuwawekea maeneo ya biashara yenye mahitaji yote muhimu.

Makamu wa Rais ambaye amekuwa mkoani Iringa kwa siku nne akihamasisha shughuli za maendeleo alisema Serikali itaendelea kuboresha na kutanua vituo vya afya kwa kuviwekea huduma bora za mama na mtoto, vyumba vya upasuaji na vyumba vya kuhifadhia maiti.

Makamu wa Rais aliwaambia wakazi wa Iringa barabara zote ambazo Ilani ya Uchaguzi ya CCM ya mwaka 2015 iliekeza ,zitajengwa kwa kiwango cha lami.

Related Articles

Back to top button

Adblock Detected

Please don't block our ads, we rely on these ads to serve you with credible contents