Wakuu wa mikoa yote Tanzania kukutana Dar Es Salaam
Wakuu wa mikoa yote nchini Tanzania wameitwa jijini Dar es Salaam kupeana mbinu mbalimbali kuhusu ugawaji vitambulisho vya wafanyabiashara wadogoalmaarufu kama Wamachinga.
Taarifa hiyo imetolewa jana Jumamosi Januari 26, 2019 Jijini Dodoma na Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI), Mhe. Seleman Jafo katika ufunguzi wa mkutano wa siku moja kwa ajili ya mikakati ya uanzishwaji wa masoko ya madini.
Waziri Jafo amesema kuwa kuna mikoa inasuasua zaidi katika zoezi hilo licha ya kuwa baadhi ya mikoa imeshafikia hadi asilimia 94.
“Niwatangazie kuwa Jumatatu tunatakiwa Dar es Salaam na Rais kwa ajili ya maelekezo zaidi na mbinu za kufanya katika kazi hii,” amesema Jafo.
Hata hivyo, Waziri Jafo hajataja mikoa inayosuasua na ile iliyofanya vizuri lakini amesema kitendo hicho kinarudisha nyuma juhudi za Rais Magufuli.