Habari

Watanzania tujifunze haya kutoka kwa Rais Magufuli

Kuna msemo ambao una tupa moyo sana sisi wanadamu kwa namna moja au nyingine ndivyo ninavyoweza kusema, Msemo huo ni ule usemao hakuna mkamilifu zaidi ya Mungu pekee katika dunia hii na umuhimu wa kitu huwezi kukiona mpaka pale kitu hicho kitakapoondoka machoni pako.

Wasomi hutumia kauli ‘Time will tell’ wakiimaanisha muda utaongea. Kwa kipindi kirefu sana Watanzania tumekuwa tukiipinga rushwa kwa kiasi kikubwa ambayo ilikuwa kansa ya maendeleo kwa nchi yetu. Lakini Mungu alisikia kilio chetu na kusema kilio cha rushwa katika taifa la Tanzania kimefika mwisho kwa kutupatia rais wa awamu ya tano Dkt John Pombe Magufuli. Simaanishi kwamba marais wa nyuma waliopita hawakuipinga rushwa hapana nawaona waliifanya kwa nafasi yao na muda walioupewa kulitumikia taifa hili.

Rais Magufuli tangu aingie madarakani amefanya vitu vingi sana kwa muda mchache. Si kweli kwamba yote anayoyafanya wengine wetu wanaweza wakayachukia lah hasha! kwasababu katika maisha pia huwezi kupendwa na wote na pia sio kila kitu unachokifanya watu wote watakipenda.

Ziara za Rais Magufuli

Rais huyu akiwa katika ziara sehemu mbalimbali za Tanzania au nchi jirani watu wengi wamekuwa wakitaka kujua kazungumzia nini katika hotuba yake na watu hutulia katika vituo mbalimbali vya televisheni kujua nini kimesemwa katika hotuba hio. N pia baada ya hotuba hiyo kuisha katika maeneo mbalimbali nchini Tanzania watu wanakuwa wakirudia kile alichokisema na kumpongeza kwa alichokisema huku wengine wakionyesha kufurahishwa na hotuba za rais huyu.

Utumbuaji majipu

Hili neno la kutumbua majipu hupenda kulitumia Rais huyu popote atakapokuwa hata akiwa katika ziara fulani au akifanya ziara ya kushtukiza sehemu ambapo akifika katika eneo hilo akiona kuna mapungufu au kuna matumizi mabaya ya fedha yeye humtumbua mtu huyo kwa kutaka asimamishwe kazi mara moja bila kutaka kusamehewa na hutumia kauli ‘Mtu akitumbuliwa hapa Dar es Salaam asije akafikiri akienda mkoa mwingine atapata kazi katika serikali hii. Hilo halipo ukifutwa kazi Dar es salaam umefutwa moja kwa moja.’ Kauli hii nadhani inawapa umakini watendaji hao sambamba na kufanya kazi kwa ufanisi kuogopa kutumbuliwa.

Baadhi ya wapinzani kusifia jitihada zake katika kupambana na rushwa

Baadhi ya viongozi wa vyama pinzani nchini wamekuwa wakifurahishwa sana na hali ya rais huyu kupinga rushwa nchini na niliwahi kumnukuu akisema, Rushwa ni kansa kwa maendeleo ya nchi.Hapa ukitaka kujua rais huyu anaichukia rushwa ukichukua ugonjwa wa Kansa jinsi ulivyo na unavyowatesa watu ndivyo utakavyoelewa ni jinsi gani amekuwa akichukizwa na baadhi ya watu ambao mpaka leo wanapenda rushwa.

Safari ya serikali kuhamia Dodoma
Ni miaka mingi tulikuwa tukisikia kuwa makao makuu ya Tanzania yapo Dodoma, lakini viongozi mbalimbali wa nchi hii wanaishi Dar es Salaam, jambo ambalo miongoni mwa watu walikuwa wakijiuliza. Ni jambo gumu sana kumhamisha mtu eneo alilokuwa akiishi siku zote au miaka yote kumpeleka sehemu ambayo huenda alikuwa akienda katika matembezi yake ya kawaida. Lakini Rais Magufuli ameweza kuwatoa baadhi ya viongozi akiwemo Waziri Mkuu na kuwahamishia Dodoma ikiwa ni sehemu ya kutaka viongozi wahamie katika makao makuu hayo. Yeye na makamu wake Bi Samia Suluhu nao wana mpango baadaye kuhamia huko.

Rais Magufuli na Kutetea wanyonge

Rais Magufuli amekuwa akiwatetea wanyonge kwa kiasi kikubwa huku akichukizwa na baadhi ya vitendo vya baadhi ya viongozi kutumia madaraka yao vibaya na kutaka viongozi wengine wajiondoe madarakani kama watashindwa kuwatetea wanyongee katika taifa hili. Katika awamu hii wanyonge wamekuwa ni watu wenye furaha ikiwemo kuachiwa huru wamachinga kufanya biashara zao. Akienda sehemu mbalimbali, amekuwa akiwatia moyo wanyonge huku akisema kuwa hata yeye ni mtoto wa mkulima hivyo matatizo ya wakulima anayatambua vilivyo. Watu wenye ulemavu wa miguu na wenye changamoto mbalimbali amekuwa akitoa sehemu ya mshahara wake kuwasaidia chochote kwaajili ya kuendesha maisha yao ya kila siku.

Serikali ya awamu ya tano

Hata katika vitabu vya dini kuna neno husema itii mamlaka iliyo juu yako. Hili lipo katika serikali hii wengi wao wamekuwa wakimtii Rais Magufuli anapotoa maagizo na baadhi yao kufuata yale anayoyataka. Kufanya ziara za kushtukiza katika maofisi mbalimbali ni kitu ambacho viongozi wa awamu hii wanakifanya. Wamekuwa si wa kukaa ofisini, wamekuwa wakuzunguka kila mahali kwaajili ya ziara ili kujua hali za wamanchi wao na changamoto wanazokutana nazo kwa namna moja au nyingine,sambamba na kuwatatulia changamoto hizo na kwa viongozi wanaofanya vibaya wamekuwa wakiwasimamisha kazi bila kuogopa.

Si kwamba serikali zilizopita zilikuwa hazina mazuri, hapana na wala si kwamba serikali hii haina mapungufu, hapana bali kwa namna moja au nyingine wanafanya vizuri katika kuliongoza taifa hili. Kikubwa ni kuwaombea ili Mungu awajaze hekima na maarifa katika kuliongoza taifa hili huku akiwapa pumzi na nguvu za kutosha kwasababu kuongoza nchi ni kitu kikubwa ambacho waweza kuona ni kitu cha kawaida kwa hali ya ubinadamu. Kikubwa tujitupe tufanye kazi kwa bidii zote ili tuweze kupata vipato vyetu kihalali.

BY: Emmy Mwaipopo

Related Articles

Back to top button

Adblock Detected

Please don't block our ads, we rely on these ads to serve you with credible contents